Waziri wa Ulinzi atoa pole vifo vya wanajeshi watatu wa Tanzania, DRC

 

Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, Mheshimiwa Dkt. Stergomena Lawrence Tax (Mb), ametoa salamu za pole kwa Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi Tanzania, Jenerali Jacob John Mkunda, kufuatia vifo vya wanajeshi watatu (3)  na wengine watatu (3) kujeruhiwa, kutokana na shambulio la Bomu  wakati wakishiriki Misheni ya Jumuiya ya Maendeleo ya Kusini mwa Afrika (SADC) nchini DRC.

Katika taarifa yake, Waziri Tax, amesema Tanzania imepoteza mashujaa hao wakiwa katika majukumu ya kutafuta amani ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo. Tunawaombea mashujaa wetu Mungu awalaze pema peponi, na kuwaponya haraka majeruhi. Mashujaa wetu watapumzishwa kwa heshima zote kwa kuzingatia taratibu za Kijeshi.

Pia, amelipongeza Jeshi la Wananchi wa Tanzania kwa kazi kubwa wanayoifanya ya kulinda amani, katika mipaka yetu na nje ya mipaka yetu kulingana na makubaliano na Itifaki za Kikanda na Kimataifa ambapo Tanzania ni mwanachama.

Aidha ametoa pole kwa ndugu, jamaa na familia kwa kuondokewa na wapendwa wao ambao wamepoteza maisha katika kutafuta amani nchini DRC.

Chapisha Maoni

0 Maoni