Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe. Angellah Kairuki
anatarajia kumwakilisha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt.
Samia Suluhu Hassan kwenye mkutano wa Kimataifa kuhusu usimamizi endelevu wa
misitu ya miombo unakaofanyika Aprili 16-18,2024 jijini Washngton DC nchini Marekani.
Mkutano huo pamoja na mambo mengine utajadili masuala mbalimbali
ikiwemo namna ya kuimarisha mashirikiano na usimamizi wa misitu ya miombo kwa
nchi wanachama za SADC, upatikanaji wa rasilimali fedha kwa ajili ya usimamizi
wa misitu ya miombo kwa nchi wanachama wa SADC, namna ya kuhama kutoka matumizi
ya nishati chafu kwenda nishati safi pamoja na jinsi ya kukabiliana na
mabadiliko ya tabianchi katika mifumo ya ikolojia na uhifadhi wa viumbe hai.
Waziri Kairuki pamoja na ujumbe wake amewasili katika Ofisi
za Ubalozi jijini Washington DC na kusaini kitabu cha wageni ambapo katika
ujumbe huo ameambatana na Mkurugenzi wa Misitu na Nyuki, Wizara ya Maliasili na
Utalii, Bw. Deusdedith Bwoyo.
Mkutano huo utafanyika chini ya Uenyekiti wa Rais wa Jamhuri ya Watu wa Msumbiji, Mhe. Filipe Jacinto Nyusi na kuhudhuriwa na Mwakilishi wa Wakuu wa Nchi kutoka nchi za SADC pamoja na Mawaziri kutoka nchi za Msumbiji, Namibia na Angola, Wabunge kutoka Malawi, Botswana,Tanzania pamoja na Maafisa Waandamizi katika Sekta ya Misitu wa nchi hizo.
0 Maoni