Mkuu wa Mkoa wa Mbeya Juma Homera amefika katika Mlima Kawetele ambao ardhi yake iliporomoka leo alfajiri na kusababisha kufukiwa kwa nyumba 20, ng’ombe wanne na kuharibika kwa miundombinu ya Shule ya Mary’s katika Mtaa wa Gombe Kata ya Itezi Halmashauri ya Jiji la Mbeya.
Tukio hilo limetokea alfajiri ya kuamkia leo ambapo chanzo
chake ni mvua zinazoendelea kunyesha mfululizo na matukio yanayofanana na haya
yamekuwa yakitukia mikoa mbalimbali ikiwemo mikoa ya Arusha na Lindi.
Akizungumza katika eneo hilo RC Homera amekanusha uvumi
unaozagaa mtandaoni ukidai kuna maafa katika tukio hilo ambapo amesema zaidi ya
hivyo vilivyotajwa aya ya kwanza hakuna madhara mengine wala maafa kama
inavyoripotiwa na baadhi ya watu.
RC Homera ameiagiza Halmashauri ya Jiji la Mbeya kufanya tathimini
juu ya waathirika hasa wale wasio na malazi ya kulala wahakikishe wanapatiwa
sehemu hizo wakati huu ambao serikali inaendelea kupambana kuhakikisha hali
inakuwa sawa katika maeneo hayo.
Pamoja na mambo mengine RC Homera amekiagiza Kitengo cha Ardhi Halmashauri ya Jiji la Mbeya kuacha kuwapimia wananchi viwanja eneo lenye changamoto hasa ya mkondo wa maji kwa kufanya kwao hivyo kutasababisha matatizo kama hayo ambayo yangeweza kuzuilika.
0 Maoni