Rais Dk. Mwinyi ahimiza kuendelea kutenda mema

 

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Alhajj Dk. Hussein Ali Mwinyi amewashukuru Masheikh na Waalimu kwa kazi kubwa ya kuendesha madarasa ya mawaidha katika Misikiti mbalimbali na Mihadhara kipindi cha Mwezi Mtukufu wa Ramadhani.

Rais Dk. Mwinyi amewashukuru wafanyabiashara waliotikia wito wa Serikali wa kutopandisha bei za bidhaa ili kuwezesha wananchi kununua bidhaa katika Mwezi Mtukufu wa Ramadhani.

Rais Dk. Mwinyi amesema hayo jana katika Baraza la Eid ukumbi wa Ziwani Chuo cha Polisi, Mkoa wa Mjini Magharibi.

Aidha, Rais Dk. Mwinyi amewahimiza waumini wa Dini ya Kiislamu kuyaendeleza mafunzo waliyopata kipindi cha Mwezi Mtukufu wa Ramadhani na kudumu kufanya mambo ya heri na kuacha kutenda maovu katika maisha ya kila siku.

Halikadhalika Rais Dk.Mwinyi amesisitiza taasisi za ZAWA, ZECO na Wizara ya Ujenzi kufanya kazi kwa ukaribu na wakandarasi wanaojenga  barabara ili kukabiliana na uharibifu wa miundombinu ya maji na umeme na huduma nyingine.

Rais Dk.Mwinyi ameliagiza Jeshi la Polisi kuhakikisha wanasimamia hali ya ulinzi na usalama wa barabarani kipindi hiki cha Sikukuu.

Vilevile amewaomba viongozi wa Dini kuendelea kuiombea Dua nchi na viongozi wake pamoja na kuendelea kudumisha amani na utulivu.

Chapisha Maoni

0 Maoni