Kamanda wa Polisi wa Mbeya SACP Benjamin Kuzaga akiwa na Waziri wa Madini Mhe. Anthony Mavunde wakionyesha dhahabu iliyokamatwa.
Jeshi la Polisi Mkoa wa Mbeya kwa kushirikiana na kikosi kazi
cha madini cha taifa linawashikilia watuhumiwa kumi wote wakazi wa Ilomba
Jijini Mbeya kwa tuhuma za kusafirisha na kutorosha vipande vya madini aina ya
dhahabu.
Kamanda wa Polisi wa Mbeya SACP Benjamin Kuzaga, amesema watuhumiwa
walikamatwa Machi 16, 2024 huko maeneo ya VETAIkulu, Jijini Mbeya wakiwa na
vipande 314 vya madini aina ya dhahabu vyenye uzito wa gramu 9,622.76 sawa na
thamani ya shilingi 1,515,621,987.03bila kuwa na kibali cha kusafirisha madini
hayo.
Pia, amasema watuhumiwa walikutwa na vifaa vingine ambavyo ni
vipimo vya dhahabu, majiko, mitungi ya gesi na kasiki ya kuhifadhi fedha.
Watuhumiwa wamekuwa wakitorosha madini hayo kupitia njia zisizo rasmi kwa lengo
la kukwepa kulipia kodi, ushuru na gharama nyingine zinazohitaji kwa
wafanyabiashara ya madini.
Jeshi la Polisi Mkoa wa Mbeya linatoa wito kwa
wafanyabiashara ya madini kufuata taratibu ikiwa ni Pamoja na kukata vibali vya
kufanya biashara hiyo na kulipa gharama zinazohitajika ili kuepuka usumbufu na
hasara pindi wanapobainika kufanya biashara bila kufuata utaratibu.
0 Maoni