Shirikisho la Soka la Tanzania (TFF) limejitenga na kauli
iliyotolewa na Waziri wa Utamaduni, Sanaa na Michezo Dkt. Damas Ndumbaro, kuhusiana
na kutumika pasipoti ya Afrika Kusini kwa mashabiki watakao vaa jezi za Mamelodi
Sundowns kwenye mechi dhidi ya Yanga.
Waziri Dkt. Ndumbaro alitoa kauli hiyo hivi karibuni, katika kile
anachoamini kuwa ni kuhamasisha uzalendo wa kuzishangilia timu za nyumbani katika
michuano ya kimataifa na kuachana na siasa za ushabiki wa Simba na Yanga.
Katika barua yao waliyoituma kwa Mkuu wa Ulinzi na Usalama wa
Shirikisho la Mpira wa Miguu Afrika (CAF), TFF wameihakikishia CAF kuwa mchezo
huo wa robo fainali ya Ligi ya Mabingwa Afrika utafanyika kwa kuzingatia kanuni
zilizopo na taratibu za kuingia uwanjani.
“Hakutatumika pasipoti kwa mashabiki wa Mamelodi Sundowns ili
kuingia katika dimba la Mkapa, na kwa vyovyote vile mechi za mpira wa miguu hazisimamiwi
na Idara ya Uhamiaji,” imesema barua hiyo iliyoandikwa na Katibu Mkuu wa TFF Kidao
Wilfred.
Barua hiyo imesema timu ya Mamelodi Sundowns maafisa wake na
mashabiki wanahakikishia ulinzi wawapo nchini kwa michezo wao dhidi ya Yanga, na hata
mashabiki wao wanaoishi Tanzania wataruhusiwa kuingia dimbani kushuhudia mchezo
huo.
Yanga imepangiwa kukutana na Mamelodi Sundowns katika hatua
ya robo fainali ya Ligi ya Mabingwa Afrika, ambapo itashuka katika dimba la
Mkapa Jijini Dar es Salaam katika mchezo wao wa wali Jumamosi Machi 30, 2024.


0 Maoni