Maalim wa Madrasa jela miaka 30 kwa kulawiti mtoto

 

Mahakama ya Hakimu Mkazi Wilaya ya Nzega mkoani Tabora imemhukumu kifungo cha miaka 30 jela, Abdallah Seleman (37) aambaye ni Mwalimu wa Madrasa katika Msikiti wa Ushirika baada ya kumtia hatiani kosa la kumlawiti mtoto wa kiume mwenye umri wa miaka 12.

Katika hukumu hiyo Hakimu wa Wilaya hiyo Nasra Mwashee amesema kuwa Mahakama imeridhika na ushahidi uliotolewa mbele ya Mahakama pasina shaka yoyote na kumuhukumu mtuhumiwa kutumikia adhabu ya kifungo cha miaka 30 jela.

Hakimu Mwashee amesema Mahakama imetoa adhabu hiyo ili iwe fundisho kwake na watu wengine wenye tabia kama hizo au wenye nia ya kufanya vitendo hivyo vya kikatili kwa watoto na kuongeza kuwa vitendo vya namna hiyo vimekuwa vikitokea mara nyingi katika wilaya hiyo.

Upande wa Mawakili wa Serikali wakiongozwa na Jenipha Mandago waliiambia Mahakama kuwa mtuhumiwa alitenda kosa hilo Oktoba 15, 2023 majira ya saa 10 jioni baada ya kuwekewa mtego kutokana na malalamiko ya mara kwa mara kutoka kwa watoto aliokuwa anawafundisha elimu ya dini katika msikiti huo.

Amessema kitendo cha kumlawiti mtoto huyo ambaye ni mwanafunzi wa shule ya msingi Imeli Wilayani Nzega kilifanyikia chooni na kumsababishia mtoto huyo maumivu makali.

Jenipha ameendelea kusema kuwa kutokana na uzito wa kosa hilo waliiomba Mahakama kutoa adhabu kali ili iwe fundisho kwake na kwa watu wengine wenye nia na tabia kama hizo kwenye jamii.

Kabla ya hukumu hiyo kutolewa hapo jana, Mahakama ilitoa nafasi ya utetezi kwa mtuhumiwa iwapo itamtia hatiani ambapo aliomba apunguziwe adhabu kwani anafamilia ya watoto wanne na mke ambao wanamtegemea.

Hata hivyo Mahakama haikuridhika na utetezi huo wa Abdallah Seleman, na kumhukumu kwenda jela kutumikia kifungo cha miaka 30, ili iwe fundisho kwa wengine wenye tabia kama hiyo.

Chapisha Maoni

0 Maoni