Sekta ya Mawasiliano ni kichocheo cha maendeleo nchini

BARA 18 (2) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inasema kuwa “Kila raia anayo haki ya kupewa taarifa wakati wote kuhusu matukio mbalimbali nchini na duniani kote ambayo ni muhimu kwa maisha na shughuli za wananchi, na pia juu ya masuala muhimu kwa jamii”. Hivyo suala la wananchi kupata habari ni muhimu kwani ni chachu ya maendeleo na pia ni takwa la kikatiba.

Ni ukweli usiopingika kuwa huduma bora za mawasiliano ni muhimu sana kwani ni kichocheo katika kuleta maendeleo ya jamii na nchi nzima kwa ujumla na umuhimu huo unadhirika kutokana na mchango wake katika nyanja za kiuchumi, kisiasa, kijamii na pia katika masuala ya ulinzi na usalama.

Vilevile, huduma ya mawasiliano ni chachu ya ukuaji wa sekta nyingine za kiuchumi kutokana na ukweli kwamba mafanikio katika sekta mbalimbali huchangiwa kwa kiasi kikubwa na uwepo wa huduma za uhakika za mawasiliano.

Hatua hiyo inatokana na maboresho makubwa yaliyofanywa na Serikali ya awamu ya sita inayoongozwa na Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan katika sekta hiyo, akiamini kwamba kupitia mawasiliano taarifa mbalimbali muhimu za Serikali na sekta binafsi zinawafikia walengwa wote wakiwemo wananchi kwa wakati na kwa ufanisi na hatimaye kuleta tija inayokusudiwa.

Januari 6, mwaka huu, Waziri Mkuu Kassim Majaliwa alizindua studio za Redio Jamii- Ruangwa ambayo itaharakisha maendeleo ya wana Ruangwa. “Tukio la leo ni hatua muhimu katika kuwapatia wananchi haki yao ya kikatiba ya kupata habari. Ni matumaini yangu kwamba Wana-Ruangwa pamoja na wananchi wa maeneo jirani watanufaika na huduma za utangazaji zitakazopatikana kupitia redio hii.”

Mheshimiwa Majaliwa alisema Sekta ya utangazaji ni muhimu sana katika dunia ya sasa ya kidigitali ambapo upashanaji wa habari umekuwa ni msingi wa ukuaji wa uchumi na kuwa chachu ya maendeleo ya mtu mmoja mmoja na Taifa kwa ujumla.

“Huu ndio msukumo wa Serikali yetu katika kuhakikisha uwepo wa miundombinu bora ya mawasiliano yatakayowezesha jamii yote ya Watanzania kupata habari muhimu za kijamii, kitaifa na kimataifa ambazo zitawapa maarifa na utayari wa kufanya shughuli mbalimbali za maendeleo ya Taifa letu.”

Alisema redio hiyo inakusudiwa kusikika katika maeneo ya Wilaya ya Ruangwa, kutokana na uwezo wa mitambo masafa yatafika hadi maeneo ya wilaya za Masasi, Liwale na Kilwa, hivyo kuwawezesha wananchi wengi zaidi kufikiwa na huduma hiyo muhimu kwani kupitia matangazo ya redio hiyo wataweza kufahamu mambo yanayoendelea katika sehemu mbalimbali nchini na duniani kwa ujumla.

Kadhalika, Mheshimiwa Majaliwa alisema ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi ya Mwaka 2020/2025; Ibara ya 125 (a) imeielekeza Serikali kuendelea kutekeleza Sheria ya Huduma za Habari na. 12 ya Mwaka 2016 ili kuhakikisha kuwa wananchi wanapata taarifa sahihi kwa urahisi zaidi na kwa wakati.

Chanzo:  Ofisi ya Waziri Mkuu

Chapisha Maoni

0 Maoni