Watoto 10 wenye matatizo ya moyo ya kuzaliwa nayo
wanatarajia kufanyiwa upasuaji wa moyo katika kambi maalumu ya upasuaji
inayofanyika katika Hospitali ya Taifa ya Moyo ya nchini Zambia.
Kambi hiyo ya upasuaji ya siku nne inafanywa na wataalamu wa
Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) kwa kushirikiana na wenzao wa hospitali
ya Taifa ya Moyo iliyopo jijini Lusaka.
Dkt. Godwin Sharau ambaye ni daktari bingwa wa upasuaji wa
moyo kwa watoto kutoka Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) alisema katika
kambi hiyo wanafanya upasuaji wa kuziba matundu ya moyo, kurekebisha valvu za
moyo pamoja na kurekebisha mishipa ya damu ya moyo ambayo haijakaa katika
mpangilio wake.
“Tuko nchini Zambia tangu jana tumeanza kufanya upasuaji
siku ya leo, tayari tumefanya upasuaji kwa watoto wawili ambao wako katika
chumba cha Uangalizi Maalumu (ICU) wanaendelea na matibabu. Hadi siku ya jumapili tunatarajia tuwe
tumefanya upasuaji kwa watoto 10”, alisema Dkt. Sharau.
“Tunaishukuru Serikali ya awamu ya sita inayoongozwa na Mhe.
Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kutusomesha wataalamu wa JKCI, kutupatia vifaa
tiba vya kisasa na kutupatia mazingira rafiki ambayo yametuwezesha kufanya kazi
zetu kiufasaha na kuweza kuwasaidia nchi za jirani ambao hawajafikai hatua kama
yetu ya kufanya upasuaji wa moyo,” alisema Dkt. Sharau.
Dkt. Sharau pia alilishukuru Shirika la Okoa Moyo wa Mtoto
(Save a Child’s Heart – SACH) la nchini Israel ambalo limewezesha kufanyika kwa
kambi hiyo kwa kutoa vifaa tiba pamoja na kuwasafirisha wataalamu wa JKCI
nchini Zambia kwenda kufanya upasuaji wa moyo kwa watoto.
Kwa upande wake daktari bingwa wa upasuaji wa moyo kwa
watoto wa Hospitali ya Taifa ya Moyo ya nchini Zambia Mudaniso Ziwa
aliwashukuru wataalamu wa JKCI kwa
kwenda katika hospitali hiyo kufanya upasuaji wa moyo kwa watoto.
“Tangu nimemaliza masomo yangu ya upasuaji wa moyo nchini Israel nimekuwa nikishirikiana na wenzangu wa JKCI kwa kujiongezea ujuzi wa kazi, mwaka jana nilikuwa JKCI kwa muda wa siku tatu kuangalia jinsi wenzangu wanavyofanya upasuaji ili siku za mbeleni nasi tuweze kufanya upasuaji wenyewe.”
“Kufanyika kwa kambi hii kunazidi kuniongezea ujuzi wa kazi
kwani najifunza zaidi, kunapunguza idadi ya watoto wanaosubiri kufanyiwa
upasuaji wa moyo nchini Zambia pia
kunaipunguzia Serikali gharama ya kuwapelea wagonjwa kutibiwa nje ya nchi,” alisema
Dkt. Ziwa.
0 Maoni