Mabadiliko ya tabia nchi yachangia kuangamiza mbegu za asili

 

Mabadiliko ya tabia nchi yameelezwa kuwa yamekuwa yakichangia kuangamiza mbegu nyingi za asili nchini, kutokana na mbegu hizo kushindwa kuhimili changamoto zinazotokana na mabadiliko hayo.

Hayo yameelezwa leo na Dk. Emmarold Mneney kutoka Agri experience wakati akiongea kwenye mafunzo ya ufahamu wa mbegu zilizoboreshwa kwa wahariri na waandishi wa habari wilayani Bagamoyo, mkoani Pwani.

“Kumekuwa na dhana potofu kuwa mbegu zilizoboreshwa zinatumika kupoteza mbegu za asili, ukweli ni kwamba mbegu za asili zinaathiriwa na mabadiliko ya tabia nchi,” alisema Dk. Mneney na kuongeza “Mbegu nyingi za asili zinashindwa kuhimili hali ya mafuriko, mvua chache pamoja na joto kali, hapo ndipo mbegu zilizoboreshwa zinapokuja kusaidia”.

Dk. Mneney amesema wanachofanya watafiki wanaozalisha mbegu zilizoboreshwa ni kurudi katika mbegu za asili kuzizidishia nguvu ili ziweze kukabiliana na changamoto za mabadiliko ya tabia nchi.

Akielezea historia ya tafiti za mbegu duniani, Dk. Mneney amesema utafiti ndio uliosaidia kupatikana kwa mbegu ya mahindi, kutoka kwenye (Mexican grass) majani ya Mexico na kuboreshwa kuwa mahindi tunayokula leo.

“Leo tusinge kuwa tunakula mahindi kusinge kuwa na utafiti wa mbegu, kwani mahindi yemetokana na tafiti iliyofanywa kutoka kwa Mexican grass (Majani ya Mexico),” alisema Dk. Mneney.

Dk. Mneney amesema mbegu zilizoboreshwa ni ufumbuzi ambao utaendelea kuwapo katika kukabiliana na mabadiliko ya tabia nchi pamoja na kuboresha uzalishaji kuendana na wakati.

Pamoja na mambo mengine, Dk. Mneney amesema mafanikio ya azma ya Tanzania kuilisha dunia yatafikiwa iwapo tu Serikali itawekeza zaidi kwenye  tafiti za uzalishaji wa mbegu zilizoboreshwa.

Mafunzo hayo ya siku mbili kuhusu uzalishaji wa mbegu bora za kilimo yameandaliwa na Brains Incorporated Limited (Media Brains) kwa kushirikiana na Alliance for a Green Revolution in Africa (AGRA).


Chapisha Maoni

0 Maoni