Bima ya Afya kwa Wote kuboresha upatikanaji huduma bora za afya

 

Serikali ya awamu ya sita kupitia Wizara ya Afya imesema kuwa itahikikisha kuwa inaboresha upatikanaji wa huduma bora za afya kwa wote kupitia mfumo wa bima ya afya kwa kuweka mfumo wa ushiriki katika skimu za bima ya afya kwa raia na wakazi wake wote.

Kauli hiyo imetolewa Bungeni jana na Waziri wa Afya Mhe. Ummy Mwalimu wakati akiwasilisha muswada wa kutunga sheria ya bima ya afya kwa wote ambapo ameeleza kuwa lengo la kuanzishwa kwa muswada huo wa Bima ya Afya kwa wote ni kutimiza wajibu wa Serikali wa kikatiba wa kuhakikisha kuwa wananchi wote wanapata huduma bora za afya bila kikwazo.

Mhe. Ummy amesema kuwa utaratibu wa kawaida wa kuchangia gharama za matibabu unachangamoto nyingi ikiwa ni pamoja na wananchi wengi kukosa huduma za afya kutokana na kukosa fedha za kugharamia matibabu papo kwa papo jambo ambalo linawapelekea wananchi kuingia katika janga la umasikini.

“Tunayo mifano iliyo hai ya wananchi ambao walilazimika kuuza mali zao ikiwemo mashamba, mifugo, vyombo vya usafiri, vifaa vya ndani na kuweka rehani mali zao ili kugharamia matibabu yao au ya wapendwa wao,” amesema Mhe. Ummy.

Mhe. Ummy amesema dhana ya huduma za afya kwa wote imejengeka katika nguzo kuu tatu ambazo ni uwezo wa kuwafikishia wananchi huduma za afya, upatikanaji wa huduma bora za afya na mfumo madhubuti wa ugharamiaji wa huduma za afya bila kikwazo cha fedha hivyo ni wakati sasa wa kila mwananchi kujiunga na bima ya afya kwa wote.

Akizungumzia upatikanaji wa bima kwa watu wasio na uwezo ameeleza kuwa Serikali ya awamu ya sita itahakikisha kuwa watu wasio na uwezo wanapata huduma bora za afya kwa kuweka mfumo maalumu ambao utagharamia bima ya afya kwa watu wa hali ya chini.

Pia ameongeza kuwa ni wajibu wa Serikali kuhakikisha wananchi wasio na uwezo wanapata huduma bora za afya na katika kuwatambua watu wasio na uwezo mapendekezo ya Serikali ni kuboresha mifumo ya utambuzi wa watu kwa kutumia Mamlaka zilizopo za takwimu za utafiti wa mapato ili kuwaweka katika utaratibu wa bima ya afya.

Chapisha Maoni

0 Maoni