Serikali yaanza kufanyia kazi mapendekezo 25 ya wafanyabiashara - Majaliwa

 

Waziri Mkuu Mhe. Kassim Majaliwa amesema Serikali imeanza kufanyika kazi mapendekezo 25 ya Kamati Maalum ya Serikali na Wafanyabiashara iliyoundwa kufuatia mgomo wa wafanyabiashara wa Soko la Kimataifa la Kariakoo.

Mhe. Majaliwa amesema kuwa Serikali imeyagawa mapendekezo hayo katika makundi ya utatuzi wa haraka makundi ya utatuzi wa kisera na makundi ambayo utatuzi wake unahitaji sheria.

Waziri Mkuu ameyasema hayo jana wakati wa kilele cha Maonesho ya Juma la Utalii na Uchumi wa Bluu (Mafia Island Festival), yaliyofanyika Mafia mkoani Pwani.

“Serikali yenu inayoongozwa na Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imefanya haya ili kuendelea kuboresha mazingira ya ufanyaji biashara,” alisema Mhe. Majaliwa.

Katika hatua nyingine, Mhe. Majaliwa amewataka Wakuu wa Wilaya kupitia kamati za mapato za wilaya wakutane na Maafisa wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) na wa Idara ya Mapato kwenye Halmashauri ili kufanya ukaguzi kwenye maeneo ya biashara na kuhakikisha risiti za EFD zinazotumika ni zile zinazotokana mashine zilizothibitishwa na kusajiliwa.

“Ni muhimu kila kiongozi anayehusika ashiriki katika kuhamasisha matumizi ya mashine za EFD na kufuatilia hali ya utoaji wa risiti kwa nidhamu kubwa bila kusababisha usumbufu na kero kwa wafanya biashara," alisema Majaliwa.

Chapisha Maoni

0 Maoni