Waziri Mkuu Mhe. Kassim Majaliwa amesema Serikali imeanza
kufanyika kazi mapendekezo 25 ya Kamati Maalum ya Serikali na Wafanyabiashara
iliyoundwa kufuatia mgomo wa wafanyabiashara wa Soko la Kimataifa la Kariakoo.
Mhe. Majaliwa amesema kuwa Serikali imeyagawa mapendekezo
hayo katika makundi ya utatuzi wa haraka makundi ya utatuzi wa kisera na
makundi ambayo utatuzi wake unahitaji sheria.
Waziri Mkuu ameyasema hayo jana wakati wa kilele cha
Maonesho ya Juma la Utalii na Uchumi wa Bluu (Mafia Island Festival),
yaliyofanyika Mafia mkoani Pwani.
“Serikali yenu inayoongozwa na Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu
Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imefanya haya ili kuendelea
kuboresha mazingira ya ufanyaji biashara,” alisema Mhe. Majaliwa.
Katika hatua nyingine, Mhe. Majaliwa amewataka Wakuu wa
Wilaya kupitia kamati za mapato za wilaya wakutane na Maafisa wa Mamlaka ya
Mapato Tanzania (TRA) na wa Idara ya Mapato kwenye Halmashauri ili kufanya
ukaguzi kwenye maeneo ya biashara na kuhakikisha risiti za EFD zinazotumika ni
zile zinazotokana mashine zilizothibitishwa na kusajiliwa.
“Ni muhimu kila kiongozi anayehusika ashiriki katika kuhamasisha
matumizi ya mashine za EFD na kufuatilia hali ya utoaji wa risiti kwa nidhamu
kubwa bila kusababisha usumbufu na kero kwa wafanya biashara," alisema
Majaliwa.
0 Maoni