Rais Samia kuzuru India tarehe 8-11 Oktoba 2023

 

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan anatarajia kufanya ziara ya Kitaifa nchini India kuanzia tarehe 8 hadi 11 Oktoba 2023 kufuatia mwaliko wa Rais wa Jamhuri ya India, Mheshimiwa Droupadi Murmu.

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. January Makamba (Mb) amewaambia waandishi wa habari jijini Dar es Salam kuwa ziara hiyo inafanyika ikiwa ni miaka minane imepita tangu ziara ya mwisho ya Kiongozi wa Tanzania nchini humo iliyofanywa na Rais wa Awamu ya Nne, Mhe. Jakaya Mrisho Kikwete mwaka 2015.

Akiongelea umuhimu wa ziara hiyo, Mhe. Waziri Makamba amesema ziara hiyo ni muhimu kutokana na historia iliyopo kati ya Tanzania na India kidiplomasia, kiuchumi, kibiashara, kidini, kiutamaduni na Maisha ya India ambayo yapo nchini Tanzania.

Amesema ziara hiyo ina lenga kuendeleza ushirikiano kati ya Tanzania na India na kuongeza kuwa katika ziara hiyo makubaliano ya kushirikiana kupitia sekta za kimkakati kama afya, viwanda, ulinzi na usalama, elimu, teknolojia ya habari na mawasiliano, uchumi wa buluu, maji, kilimo, biashara na uwekezaji pamoja na kutangaza fursa za biashara na uwekezaji za Tanzania ili kuvutia wawekezaji na wafanyabiashara wa India waje nchini.

Akiongelea faida zinazotarajiwa kupatikana kutokana na ziara hiyo, Mhe. Makamba amesema katika ziara hiyo inatarajiwa kuwa hati mbalimbali za makubaliano zitasainiwa na hivyo kuleta tija katika maeneo ya Mafunzo ambapo Maelfu ya Watanzania watapata nafasi za mafunzo na kujengewa uwezo katika nyanja mbalimbali nhini India na kuongeza kuwa India imeazimia kutoa ufadhili na fursa za mafunzo zaidi ya elfu moja katika fani mbalimbali.

Amesema ziara hiyo itawezesha maendeleo na mapinduzi ya kidijitali na inatarajiwa kuwa India itaanzisha kiwanda cha mitambo ya kuunda bidhaa za kielektroniki na kuanzisha mifumo ya kutumia Akili Tarakilishi nchini.

Amesema kuwa ziara hiyo inatarajia kuinua ubora wa huduma za Afya nchini ambapo taasisi ya upandikizaji wa figo na kiwanda cha kutengeneza chanjo za wanyama na binadamu zenye ubora vitaanzishwa, kuwezesha ushirikiano mkubwa kati ya Hospitali zetu na Hospitali za India zinazotoa huduma za afya kwa mifumo ya Tiba Asilia pamoja na kuwezesha upatikanaji wa dawa zenye ubora kwa gharama nafuu.

Akiongelea faida itakazopata sekta ya Kilimo Mhe Waziri Makamba amesema kupata masoko kwa mazao ya kilimo kwa kuwa tunazalisha mbaazi, korosho na mazao mengine ambayo India ni sehemu ya soko pamoja na kuinua na kuongeza biashara ya mazao yanayozalishwa nchini hususan mbaazi, kunde, parachichi na ufuta.

“Tukumbuke kuwa bei ya mbaazi mwaka huu imekuwa kubwa hii ni kwa sababu India wamenunua mbaazi kwa wingi kwahiyo ziara hii itahakikisha soko la mbaazi linakuwa kubwa na linaendelea kuwepo sio msimu huu lipo au msimu ufuatao linakosekana,” alisema Mhe. Waziri.

Amesema ziara hii pia itawezesha uwekezaji wa moja kwa moja kwa kuvutia uwekezaji kutoka kwa wafanyabiashara wakubwa na kampuni mbalimbali kutoka India; kuimarisha Ulinzi na Usalama katika usafiri wa majini ambapo India inatarajia kuanzisha karakana ya utengenezaji wa vyombo vya majini na ukarabati.

Mhe. Waziri Makamba amesema katika ziara hiyo Mhe. Rais Samia anatarajiwa kufungua Kongamano la biashara na uwekezaji kati ya Tanzania na India

litakalowezesha wafanyabiashara na kampuni mbalimbali za nchini kupata fursa za kufanya biashara ya bidhaa zao na uwekezaji nchini India na kushiriki mikutano ya uwili na majadiliano kati ya wafanyabiashara wa Tanzania na wafanyabiashara wa India pamoja na kushuhudia ubadilishinaji wa Hati za Makubaliano kati ya Sekta Binafsi za Tanzania na India.

Akiongelea kuhusu ushirikiano kati ya Tanzania na India, Mhe. Waziri Makamba amesema Uhusiano huo uliasisiwa na waasisi wa mataifa hayo Baba wa Taifa, Hayati Mwalimu Julius Kambarage Nyerere na Hayati Mahatma Gandhi ulitokana na falsafa za viongozi hao ambao walipenda kutafuta suluhu ya amani pasipokuwa na umwagaji damu.

Akiongelea yatakayojiri katika ziara hiyo Mhe. Waziri Makamba amesema Mhe. Rais Samia akiwasili nchini India atapokelewa rasmi tarehe 9 Oktoba, 2023 na Rais wa India, Mhe. Droupadi Murmu ambaye ataambatana na Mhe. Narendra Modi, Waziri Mkuu wa Jamhuri ya India na kufanyiwa sherehe za mapokezi rasmi ambayo yatahusisha gwaride rasmi na kupigiwa mizinga 21.

Baada ya mapokezi hayo, Mhe. Rais Samia atakuwa na mazungumzo ya faragha na Mhe. Waziri Mkuu Modi na kufuatiwa na mazungumzo ya uwili kati ya ujumbe wa Tanzania na India na watashuhudia ubadilishanaji wa Mikataba na Hati za Makubaliano kati ya Tanzania na India na baadaye kuzungumza na waandishi wa habari kuelezea muhtasari wa mazungumzo yao.

Jioni ya siku hiyo Mhe. Rais Samia atazungumza na mwenyeji wake, Rais wa India, Mhe. Droupadi Murmu na kushiriki dhifa ya kitaifa itakayoandaliwa kwa heshima yake na mwenyeji wake katika Ikulu ya India.

Chapisha Maoni

0 Maoni