Dk. Salim ni Mtanzania mahiri na mashuhuri- Rais Samia

 

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan, amesema Dk. Salim Ahmed Salim ni Mtanzania mahiri na mashuhuri aliyetoa mchango mkubwa katika maendeleo ya Tanzania na bara zima la Afrika.

Rais Samia ameyasema hayo leo katika hafla ya kuzindua Tovuti ya Hifadhi ya Nyaraka za Kumbukumbu za Kidigitali za Dk. Salim Ahmed Salim, iliyofanyika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNICC) jijini Dar es Salaam.

Amesema kwamba katika nyanja ya Kidiplomasia Dk. Salim aliliwakilisha vyema taifa la Tanzania, katika nchi mbalimbali zikiwamo Misri, India, China, Marekani, katika Umoja wa Mataifa na Umoja wa Nchi Huru za Afrika (AU) na kwingineko.

“Dk. Salim alijitahidi sana kuhuisha mahusiano mazuri baina ya Tanzania na nchi nyingine pamoja na taasisi alizohudumu, akiwa balozi wa Tanzania nchini India alihamasisha serikali ya India ya Waziri Mkuu wa wakati huo Indra Gandhi kuanzisha viwanda vidogo vidogo nchini,” alisema Rais Samia.

Aidha, Rais Samia amesema uwakilishi mahiri wa Dk. Salim nchini China uliimarisha sana mahusiano baina ya nchi hizi na kupelekea Baba wa Taifa Hayati Julius Kambarage Nyerere kuwa rais wa kwanza kutoka Afrika kufanya ziara nchini China.

“Mahusiano mazuri haya baina ya China na Tanzania yalisaidia kufanikisha uanzishwaji wa viwanda mbalimbali kikiwamo kiwanda cha nguo cha Urafiki (Urafiki Textile Industries) na baadae ujenzi wa reli ya TAZARA nchini,” alisema Rais Samia.

Amesema wakati Dk. Salim alipokuwa mwakilishi wa Tanzania kwenye Umoja wa Mataifa alichangia kwa kiasi kikubwa katika harakati za ukombozi na mpango wa kuirudishia China kiti chake cha kudumu kwenye Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa.

“Mpango wa kuirudishia China kiti cha kudumu kwenye baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa ulimugharimu Dk. Salim pamoja na sababu zingine za kukosa kwake nafasi ya Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa,” alisema Rais Samia na kuongeza, “Pamoja na sababu zingine za kuambiwa kuwa mweusi hawezi kushika nafasi hiyo, lakini kulikuwa na sababu zingine moja wapo likiwa hili la Dk. Salim kusimama kidete na nchi ya China.”

Amesema kwa upande wa nchini, Dk. Salim amelitumikia taifa katika nafasi mbalimbali kama vile Waziri Mkuu, Waziri wa Mambo ya Nchi, Waziri wa Ulinzi na nafasi zingine alizopewa na alichapa kazi kwa moyo wake wote na kudhihirisha uongozi wake uliojaa uadilifu.

Katika hafla hiyo Rais Samia ametangaza kubadilisha jina la Chuo cha Diplomasia nchini na kukipa jina la Waziri Mkuu Mstaafu Dk. Salim Ahemd Salim, ambapo sasa Chuo hicho kitakuwa kinaitwa Dr. Salim Ahmed Salim Centre for Foreigh Relations.

Chapisha Maoni

0 Maoni