Mwanamke Mariam Paul mwenye wa miaka 30 amejikuta katika
wakati mgumu baada ya kummwagiwa maji ya moto na mke mwenzake ajulikaye kwa
jina la Vumilia Kasomelo mwenye umri wa miaka 32 kutokana na kile kinachodaiwa
kuwa ni wivu wa mapenzi.
Inadaiwa kuwa Mariam Poul alienda katika kijiji cha Lugata
kilichopo katika kisiwa cha Kome kuhudhuria msiba wa baba mkwe wake, ndipo
akakutana na mke mwenzake huyo aliyepatwa na hasira na kummwagia maji ya moto
usiku wa manane wakati alipokuwa amelala.
“Hadi sasa sijui shida ni nini hadi yeye kunimwagia maji ya
moto mimi niko kwangu na yeye anaishi kwake tumekutana tu msibani kumzika baba
mkwe wetu nashangaa yeye kuniunguza na maji ya moto,” amesema Mariam huku akiugulia
machungu.
Ndagabwene Evarist mwenye umri wa miaka 33 ni mume wa
wanawake hao amesema tukio hilo limemsikitisha sana kufuatia kutokea wakati wa
msiba wa baba yake mzazi na kuiomba radhi jamii kwa tukio hilo na kudai
wanawake hao hawajawahi kuonana siku hiyo ilikuwa ya kwanza ndipo tukio hilo
likatokea.
“Nilikuwa nimechukua jukumu la kumuadhibu mke wangu mkubwa
lakini jamii ikanizuia na kusema niache sheria itachukua mkondo wake” amesema
Evarist.
Mwanamke anayedaiwa kufanya tukio hilo ambae ndiyo mke mkubwa
Vumilia Kasomelo mwenye umri wa miaka 32 ambae ni mama wa watoto 6, alisema
baada ya kumuona mke mwenzake alishikwa na hasira na kupelekea kufanya kitendo
hicho cha kummwagia maji ya moto usiku alipokuwa amelala.
Kwa upande wake Ofisa Mtendaji kata ya Lugata Rafael Jangole
amethibitisha kutokea kwa tukio hilo na kusema mtuhumiwa amekiri kutenda kosa
hilo huku akisema kwamba kilichopelekea kufanya hivyo ni wivu wa mapenzi.
"Tunamshikilia kwa sasa huku tukiandaa taratibu za
kumpeleka polisi kwa ajili ya taratibu zingine, Mariamu Paul ameumia sehemu
mbalimbali za mwili wake huku mkono wa kushoto ukiwa umeungua zaidi,” amesema
Jangole.
Ndagabwene Evarist akiwa na mke wake mdogo Mariam Paul aliyemwagiwa maji ya moto na mke mkubwa Vumilia Kasomelo, ambaye anashikiliwa kwa kufanya kitendo hicho cha kikatili.
0 Maoni