Hospitali ya Taifa Muhimbili Mloganzila hadi sasa imetoa
huduma ya kupunguza uzito kwa watu 128 wenye uzito uliopitiliza kwa kutumia
puto maalum (intragastic balloon) , ambapo huduma hiyo pamoja na kupunguza
uzito imekuwa na mafanikio makubwa ikiwemo kuwawezesha wateja hao kutekeleza
majukumu yao kwa ufanisi tofauti na ilivyokuwa awali.
Kauli hiyo imetolewa na Kaimu Mkuu wa Idara ya Upasuaji
MNH-Mloganzila Dkt. Erick Muhumba na kubainisha kuwa kati ya watu hao 128
waliofanyiwa huduma hiyo wanawake wanne (4) wamefanikiwa kupata ujauzito ambapo
mmoja wao alikaa zaidi ya miaka sita bila kupata ujauzito kutokana na tatizo la
uzito uliopitiliza.
Dkt. Muhumba ameongeza kuwa zaidi ya watu 12 wameondolewa
puto hilo kutokana na uzito wao kupungua na wachache wameondolewa kutokana na
maudhi madogo madogo waliyoyapata kutokana na kuwekewa puto hilo hivyo
kupelekea kuliondoa.
“Wapo baadhi ya wateja wetu takribani wanne tuliwawekea puto
lakini tumelazimika kuliondoa kutokana na maudhi madogo madogo ikiwemo
kutapika, lakini wengi wao huduma hii imekuwa rafiki na yenye mafanikio makubwa
na wapo ambao wametoa baada ya uzito kupungua” amesema Dkt. Muhumba
Dkt. Muhumba amefafanua kuwa wapo ambao wameongeza maji au
kupunguza maji kwenye puto kulingana na mahitaji ya wateja, ametoa mfano kuwa
miongoni mwa waliongezewa maji kwenye
puto kwa lengo la kuendelea kupunguza uzito ni msanii na balozi wa puto
Mloganzila Bw. Peter Msechu.
Kwa upande wake msanii na balozi wa puto Bw. Peter Msechu
amesema kwa kipindi cha miezi sita amepunguza takribani kilo 17 kutoka 144
alizokuwa nazo awali na ameona umuhimu wa kuongeza maji kwenye puto kutokana na
kuwa na kasi ndogo ya uzito kupungua.
Msechu ameongeza kuwa tangu awekewe puto ameweza kufanya
majukumu yake kwa muda mrefu bila kuchoka, pia amebainisha kuwa uzito wake
haujapungua kwa kasi kama alivyotarajia kutokana na kutofanya mazoezi kama
alivyoshauriwa na wataalamu hali iliyotokana na ratiba yake kusongwa na
majukumu mengi ya kitaifa.
0 Maoni