Hifadhi za taifa zatakiwa kujitangaza kimkakati

 

Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii Mhe. Mary Masanja (MB) ameelekeza watumishi wa Shirika la Hifadhi za Taifa Tanzania (TANAPA) kuzitangaza kimkakati Hifadhi za Taifa ambazo bado hazijaweza kujitegemea kimapato, zijitegemee ili ziweze kuchangia katika pato la Taifa.

Ameyasema hayo leo tarehe 11.07.2023 alipotembelea Banda la Shirika la Hifadhi za Taifa Tanzania katika Maonesho ya 47 ya Kimataifa ya Biashara yanayoendelea katika viwanja vya Kurasini jijini Dar es Salaam,katika maelezo yake alizitaja hifadhi hizo kuwa ni Burigi-Chato, Rumanyika- Karagwe, Kitulo, Katavi na Ibanda - Kyerwa.

 Aidha, Mhe.Masanja amewataka TANAPA kushirikiana na Mawakala wa Utalii nchini kuandaa safari za kutembelea hifadhi hizo kwa gharama nafuu ili kukuza utalii wa ndani. Alitolea mfano kuwa uhamasishaji huo pia, ujikite katika taasisi za Serikali na zisizo za kiserikali, wageni wakaazi na wasio wakaazi “expatriates” walioko katika maeneo ya migodi kama Geita na kwingineko.

"Ili kuongeza idadi ya watalii watakao tembelea hifadhi zetu niwaelekeze TANAPA kukaa na wadau na kuangalia njia bora za kukuza utalii wa ndani na kupanua wigo wa kutangaza utalii wa ndani  kwa ajili ya kulifikia soko kubwa zaidi, pia shirikianeni na  vijana wenye taaluma za uhifadhi na utalii wazijue fursa za uwekezaji zilizopo katika hifadhi za taifa wawekeze na kunufaika nazo,” aliongeza Mhe. Masanja.

Hata hivyo, aliwataka wadau wa utalii kushirikiana na taasisi zilizo chini ya Wizara ya Maliasili na Utalii kuandaa vifurushi vya bei nafuu kwa nyakati za Maonesho na sikukuu kuvutia wananchi wengi zaidi kutembelea vivutio hivi adimu.

Maonesho hayo ya Kimataifa ya Biashara yanayoendelea jijini Dar es Salaam yalianza takribani siku 11 zilizopita na yanatarajiwa  kuhitimishwa tarehe 13.07.2023.

Na. Jacob Kasiri - Dar es Salaam.

Chapisha Maoni

0 Maoni