Simba wawili waingia vijiji vinne Muheza na kula mifugo usiku

 


Wanavijiji wa vijiji vinne vya Mpapayu, Tanganyika, Mlingano na Kwalubuye wilayani Muheza mkoani Tanga wamekuwa wakiishi kwa hofu kufuatia uwepo wa simba wawili walioingia Muheza kutokea Masaika, ambao wamekuwa wakila mifugo yao usiku.

Taarifa ya Afisa Maliasili Muheza, Obadia Msemo, imeeleza kuwa tarehe 28 na 29 kwa upande wa Masaika unaopakana na Muheza simba hao walikula punda mmoja na mbuzi mmoja, na tarehe 30 walibainika kuwepo upande wa Muheza baada ya kuonekana kwa nyayo zao.

Taarifa hiyo imeendelea kueleza kwamba tarehe 30 kuamkia tarehe 31 katika kijiji cha Mpapayu aliliwa punda mmoja, jana tarehe 01.06.2023 majira ya asubuhi nyayo za simba zilionekana katika kijiji cha Tanganyika kata ya Lusanga, ambapo baadaye jioni walipokea taarifa za uwepo wao kitongoji cha Kizota kijiji cha Mlingano.

Pia usiku wa kuamkia leo tarehe 02 kitongoji cha Mshukuruni kijiji cha Kwalubuye Mwenyekiti wa Kijiji hicho ameripoti kuwa usiku ng'ombe mmoja ameliwa. “Hivyo, Hali bado si salama kwa kuwa TAWA hawajafanikiwa kukutana na simba, pia mashambulizi yao yamekuwa ya wakati wa usiku”.

Kutokana na hali hiyo Mkuu wa Wilaya Muheza amesisitiza wanavijiji kuendelea kuchukua tahadhari katika kipindi hiki, wakati huu ambapo wataalamu wa wanyamapori kutoka TAWA waliopo Muheza na wengine wanaotegemewa kutoka TAWIRI, wakiwasaka simba hao.

Chapisha Maoni

0 Maoni