Prof. Janabi asisitiza watu kufanya uchunguzi wa afya

Mkurugenzi Mtendaji Hospitali ya Taifa Muhimbili, Prof. Mohamedi Janabi, amewashauri wataalamu wa afya kuweka msisitizo katika kutoa elimu kwa jamii kuhusu umuhimu wa kufanya uchunguzi wa afya zao ili waweze kujua hali zao na kuanza kupata matibabu mapema na kuepuka madhara zaidi.

Prof. Janabi ameyasema hayo wakati wa kongamano la kitaaluma lililofanyika leo na kuhudhuriwa na Daktari Bingwa wa Upasuaji kutoka HeathCare Global (HCG) Cancer Center ya Ahmedabad -India, kongamano hilo limelenga kubadilishana uzoefu wa matibabu ya saratani ya matiti baina ya kituo hicho na MNH-Mloganzila.

Prof. Janabi ameongeza kuwa uongozi wa Hospitali ya Taifa Muhimbili-Upanga na Mloganzila hivi karibuni utaeandesha zoezi maalumu la kufanya uchunguzi wa afya za watumishi wake ambapo utafanya uchunguzi wa saratani ya matiti na saratani ya shingo ya kizazi wa wanawake na saratani ya tezi dume kwa wanaume.

“Tumeamua kufanya uchunguzi wa afya za watumishi kwakuwa mara nyingi tumekuwa tukiweka kipaumbele katika kuchunguza afya za jamii na sisi kujisahau, umuhimu wa uchunguzi huu wa hiyari kwa watumishi ni kubaini kama mtu ana maradhi haya ili aweze kuanza matibabu mapema na kuepuka madhara zaidi” amebainisha Prof. Janabi.

Prof. Janabi amesisitiza wataalamu kuendelea kumhudumia mgonjwa kwa pamoja (teamwork) ili kuweza kushauriana na kutoa matibabu stahiki na kwa wakati badala ya kila mtaalamu kumuona mgonjwa kwa wakati wake.

Kwa upande wake Daktari Bingwa kutoka HGC Cancer Center ya India, Dkt. Tanay Shah amesema matibabu ya saratani duniani yanaendana na mabadiliko ya teknolojia hivyo ili kuendelea kutoa huduma bora kwa wateja ni vyema kuendelea kujifunza na kubadilishana uzoefu miongoni mwa wadau wa sekta ya afya.

Ameongeza kuwa hospitali yao imekuwa ikishirikiana na hospitali mbalimbali nchini kwa kuleta madataktari na wataalamu wengine wa afya kuja kufanya kazi katika hospitali hizo kwa lengo la kubadilishana uzoefu na ujuzi walionao.

Naye, Daktari Bingwa wa Upasuaji MNH-Mloganzila, Dkt. David Antanamsu amefafanua kuwa saratani ya matiti ni saratani ya pili Duniani kwakuwa inaongoza kwa asilimia 15 ya saratani zote zinazowakumba wakina mama.

Ameongeza kuwa matibabu ya saratani ya matiti kwa wakina mama ikihusisha kurekebisha titi bila kuliondoa inafanyika MNH-Mloganzila na kuwasihi wenye changamoto hizo kufika kwa matibabu.

Chapisha Maoni

0 Maoni