Hii hapa Bajeti ya Shilingi Trilioni 44.39

 

Waziri wa Fedha Na uchumi Dk Mwigulu Lameck Nchemba amewasilisha Bajeti Kuu ya Serikali kwa mwaka mwaka wa fedha 2023/24 inaonesha kuwa jumla ya shilingi trilioni 44.39 zinatarajiwa kukusanywa na kutumika.

Akiwasilisha bajeti hiyo leo katika Bunge la 12, mkutano wa 11 kiako cha 49 Dk. Nchemba amesema kwamba jumla ya mapato ya ndani yanatarajiwa kuwa shilingi trilioni 31.38, sawa na asilimia 70.7 ya bajeti yote.

Ameongeza kwamba kwamba kati ya mapato hayo, mapato yatakayokusanywa na Mamlaka ya Mapato Tanzania yanakadiriwa kuwa shilingi trilioni 26.73 na mapato yasiyo ya kodi (Wizara, Idara, Taasisi na Mamlaka za Serikali za Mitaa) yanakadiriwa kuwa shilingi trilioni 4.66.

Amesema misaada na mikopo  nafuu kutoka kwa Washirika wa Maendeleo inatarajiwa kuwa shilingi trilioni 5.47, ambapo pia Serikali inatarajia kukopa shilingi trilioni 5.44 kutoka soko la ndani ambapo shilingi trilioni 3.54 ni kwa ajili ya kulipia hatifungani na dhamana za Serikali zinazoiva na kiasi cha shilingi trilioni 1.90 ni kwa ajili ya kugharamia miradi ya maendeleo.

Vilevile, Serikali inatarajia kukopa shilingi trilioni 2.10 kutoka soko la nje kwa masharti ya kibiashara kwa lengo la kuongeza kasi ya utekelezaji wa miradi ya maendeleo.

Dk. Nchemba amesema katika mwakawa fedha 2023/24, Serikali inapanga kutumia jumla ya shilingi trilioni 44.39 kwa matumizi ya kawaida na maendeleo.

Ameongeza kuwa kati ya kiasi hicho, shilingi trilioni 30.31 zimetengwa kwa ajili ya matumizi ya kawaida, ikijumuisha: shilingi trilioni 12.77 kwa ajili ya ulipaji wa deni la Serikali na gharama nyingine za Mfuko Mkuu; shilingi trilioni 10.88 kwa ajili ya mishahara ikiwemo nyongeza ya mshahara, upandishaji wa madaraja na ajira mpya.

Pia shilingi trilioni 1.14 ni ruzuku ya maendeleo kwa ajili ya kugharamia elimumsingi na sekondari bila ada pamoja na mikopo ya wanafunzi elimu ya juu; shilingi trilioni 5.52 ni kwa ajili ya matumizi mengineyo (OC).

Aidha, Dk. Nchemba amesema matumizi ya maendeleo yanatarajiwa kuwa shilingi trilioni 14.08. Kiasi hicho kinajumuisha gharama za utekelezaji wa miradi mbalimbali katika ngazi ya Serikali Kuu na Mamlaka za Serikali za Mitaa.



Chapisha Maoni

0 Maoni