Mei 3,2023 ilikuwa ndiyo siku ya mwisho ya pumzi ya Mganga Mfawidhi wa Kituo cha Afya Nyangoto kilichopo Kata ya Nyamongo, Tarime Vijijini Dk Isack Daniel Athuman.
Hii ni baada ya kuuwawa kwa kukatwakatwa Mapanga na Watu Wasiojulikana wakati akitoka kituo chake cha kazi akirejea nyumbani.
Taarifa ya kifo chake inaeleza wakati anarudi nyumbani, alikutana na watu waliosimamisha pikipiki yake na kumshambulia kwa mapanga.
Kwa mujibu wa rais MAT Dk Elisha Osati akimuelezea marehemu alisema kuwa ni mmoja wa Madaktari 1000 waliopewa ajira na Rais hayati John Magufuli katika maadhimisho ya siku ya Madaktari 2020”.
Osati alisema marehemu Isack alikuwa tayari kuwahudumia wananchi vijijini na alikua na kawaida ya kujitoa hata muda wa ziada.
Maziko yake tayari yamefanyika kijijini Kaselya, Ndago, wilaya ya Iramba, mkoani Singida huku hatua zaidi zikitakiwa kuchukuliwa na kukamatwa waliohusika na mauwaji.
Taarifa ya kitengo cha Mawasiliano Wizara ya Afya iliyosainiwa na Aminiel Eligaesha Mei 6,2023 inasema kuwa Wizara inalaani vikali kitendo hicho cha kuuwawa kwa mwanataaluma huyo wa udaktari.
Dk Isack baada ya kuhitimu shahada ya udaktari Chuo Kikuu cha Mtakatifu Francisko ndaki ya Afya na Sayansi Shirikishi (SFUCHAS) na mafunzo kwa vitendo aliajiriwa kituo cha afya Nyangoto kata ya Nyamongo, Tarime vijijini ambako amefanya kazi kwa miaka miwili kama Mganga Mfawidhi.
Waziri wa afya Ummy Mwalimu ni miongoni mwa viongozi wa serikali waliolaani tukio hilo na kuvitaka vyombo vya dola kufanya uchunguzi na kuwabaini waliohusika na mauwaji hayo.
Msemaji wa serikali Gerson Msigwa naye akaguswa na tukio hilo na kuandika kupitia mtandao wa instagram
0 Maoni