Wanawake nchini wametakiwa kuchukua tahadhari ya ugonjwa wa saratani ya mfuko wa mayai ya uzazi (ovari) ambao umeanza kujitokeza kwa kasi haswa kwa wanawake wenye umri wa miaka 30 kuendelea.
Daktari bingwa wa saratani kutoka hospitali ya Benjamin Mkapa Caroline Mrema amesema dalili zake ni pamoja na kuvimba kwa tumbo, kupungua uzito kwa kasi,maumivu ya nyonga, kukosa hamu ya kula,ikiwa kubwa zaidi mgonjwa anaweza kupata maumivu ya mgongo kwenda haja ndogo mara kwa mara kutokana na mkandamizo wa uvimbe kwenye kibofu cha mkojo
Dk Mrema amesisitiza kufanya uchunguzi wa mara kwa mara ili kuweza kupata matibabu sahihi na ugonjwa huo huwapata wanawake wengi haswa waliofikia katika ukomo wa hedhi.
Kwa upande wake daktari bingwa kutoka taasisi ya saratani ya Ocean Road Dk Faraja Kiwanga amesema taasisi hiyo imekuwa ikifanya utafiti mbalimbali ili kubaini chanzo cha ongezeko la saratani hiyo.
Dk Kiwanga amesema wanawake wenye umri wa miaka 35 kuendelea na wamechelewa kuzaa wapo kwenye hatari zaidi ya kupata saratani ya ovari.
Akihojiwa na Tbc1 amesema kinga pekee ni kufanya uchunguzi ambao hufanywa kwa kupima damu na njia ya kwanza ya matibabu yake ni upasuaji na kuondolewa mfumo wake wa uzazi kama itakuwa imeongezeka kwenye kiwango chake ambacho hakijategemewa.
Baada ya hapo mgonjwa atapata tiba kemia ambazo zitasaidia kama mgonjwa ana viashiria vya saratani vimebaki kwenye mfumo vinaweza kushambuliwa kwa kutumia tekinolojia ya kemotheraphy.
Amesema kwa makadirio kwa siku wanaweza pokea mgonjwa mmoja ila kwa mwezi ni kati ya sita au tisa lakini haipo katika zile saratani zinazoonekana mara kwa mara.
Miongoni mwa sababu kubwa zinazotajwa ni uzito uliokithiri kwahiyo amewataka wanawake kufanya mazoezi na kuacha mtindo mbaya wa ulaji vyakula.
Mei 8 kila mwaka dunia huadhimisha siku ya saratani ya mfuko wa kizazi (ovari)ugonjwa ambao unatajwa kushambulia idadi kubwa ya wanawake duniani.
4 Maoni