Baba mzazi wa aliyejirusha ghorofani Makumbusho afunguka mazito kifo cha mwanaye


Baba mzazi wa Marehemu Joel Misesemo aliyejirusha katika jengo la ghorofa la Derm Plaza lililopo Makumbusho, ameeleza mapito ya mwanaye kabla ya umauti.

Akizungumza jijini Dar es Salaam wakati akitoa taarifa kuhusu maziko ya mtoto wake baba mzazi wa marehemu, Mzee Mattson Misesemo amesema marehemu Joel  alikuwa anasumbuliwa na ugonjwa wa kiharusi kwa muda mfupi lakini alipata matibabu na kuendelea na shughuli zake kama kawaida.


Akizungumza kwa uchungu Mzee Mattson amesema Joel hakuwahi kumtaarifu kuwa na changamoto yeyote kuhusu maisha yake kwani alikuwa anaishi na familia yake na kudai  hajui kilimpata nini hadi akaamua kujirusha ghorofani.


Jeshi la polisi 

Kamanda wa Jeshi la Polisi  Kanda Maalumu ya Dar es Salaam SACP Muliro Jumanne Muliro alithibitisha kifo cha Joel Misesemo aliyejirusha ghorofani Makumbusho.


Taarifa ya SACP Muliro ilieleza  uchunguzi wa awali unaonesha kuwa marehemu alionekana katika jengo hilo tarehe 23, Mei 2023 majira ya saa 11:40 alifajiri na alimwambia mlinzi wa zamu kuwa anaenda kufanya ibada kwenye msikiti uliopo ghorofa ya 15 ndani ya jengo hilo, hata hivyo muda mfupi baadaye alijirusha kutoka juu ghorofani na kuanguka chini.


Majirani wafunguka

Baadhi ya majirani waliomzungumzia wamesema Joel alikuwa ni mtu wa watu, alijichanganya na kuongea na kila mtu  mtaani na kuwa marehemu enzi za uhai wake katika ghorofa ambayo umauti ulimkuta alikuwa akienda kufanya mazoezi kipindi alivyokuwa mgonjwa.


Janeth Andendekise, ni binti aliyelelewa na marehemu tangu mwaka 2016 amesema baada  ya wazazi wake kufariki alipitia  changamoto mbalimbali za kimaisha ikiwemo kuumwa lakini alipokutana na Joel alimpokea na kukubali kuishi naye mpaka alipoweza kuanza maisha ya kujitegemea.


Janeth anasema mara ya mwisho kuzungumza na marehemu  ilikuwa Jumatatu akiwa visiwani Zanzibar anapofanya shughuli zake za biashara na kumtaarifu kuwa amepata mchumba na yupo mbioni kwenda kumtambulisha.


Anasema hukuwa anafahamu kama marehemu alikuwa akisumbuliwa na ugonjwa wa kupooza mpaka mke wa marehemu ambaye anamwita bibi alipomueleza kuwa alipooza kwa zaidi ya mwezi mmoja.



Kuzikwa Kinondoni 

Mwili wa marehemu Joel unatarajiwa kuzikwa Ijumaa katika makaburi ya Kinondoni jijini Dar es Salaam.


Marehemu Joel enzi za uhai wake alikuwa ni mshehereshaji na mhamasishaji   alikuwa na mke hakuwahi kufanikiwa kuwa na mtoto lakini aliwalea watoto wa watu wengine wanne waliopitia matatizo mbalimbali.

Chanzo:Mwananchi/globaltv/tanpoltz

Chapisha Maoni

0 Maoni