Wizara ya fedha, Tanzania bara na Zanzibar zabadilishana uzoefu

 

Na. Martha Mbena na Jordan Mbwambo, WF, Dodoma 

Watumishi wa Wizara ya Fedha ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Idara ya Sera za Ununuzi wa Umma na wa Wizara ya Fedha na Mipango, Zanzibar, Idara ya Usimamizi Sera za Umma, wamebadilishana uzoefu kuhusu matumizi ya Daftari la Kielektroniki la Taarifa za Maafisa Ununuzi na Ugavi Serikalini.

Watumishi hao wamekutana jijini Dodoma kwa ajili ya kujifunza namna ya usanifu na ujenzi wa  Daftari la Kielektroniki la Taarifa za Maafisa Ununuzi na Ugavi Serikalini (Procurement and Supplies Personnel Information System – PSPIS) ambalo hutumika kama zana ya utekelezaji wa matakwa ya Kifungu  cha  7(j) cha Sheria ya Ununuzi wa Umma Na. 10 ya Mwaka 2023, kinachoipa Wizara jukumu la kushauri kuhusu muundo, uteuzi wa Wakuu wa Vitengo vya Usimamizi wa Ununuzi na Ugavi, na kupendekeza uhamisho wa watumishi wa ununuzi na ugavi.

Akizungumza wakati wa kikao kazi hicho, Kaimu Kamishna wa Sera za Ununuzi wa Umma, Wizara ya Fedha, Bw. Alex Haraba, amesema kuwa Mfumo wa PSPIS ni nyenzo muhimu inayosaidia Serikali kuwa na taarifa sahihi za watumishi wanaotekeleza majukumu ya ununuzi wa umma na ugavi.

"Matumizi ya Mfumo huo yanawezesha taarifa za maafisa wa ununuzi na ugavi kukusanywa na kusimamiwa kwa ufanisi, hatua inayosaidia Serikali kufanya maamuzi kwa kuzingatia taarifa sahihi na zinazopatikana kwa wakati," amesema Bw. Haraba.

Amesema taarifa hizo ni muhimu katika kupanga rasilimali watu, kutambua mahitaji ya kada, kujenga uwezo wa watumishi na kutoa ushauri wa kisera na kiutendaji.

Aidha, daftari la watumishi wanaofanya kazi za ununuzi na ugavi katika Vitengo vya Usimamizi wa Ununuzi (PMUs) ni nyenzo ya kiutawala inayolenga kuiwezesha Serikali kuwa na kumbukumbu sahihi, zilizohakikiwa na zinazosasishwa kuhusu watumishi hao.

Pia, katika kikao kazi hicho, wataalamu wa Idara ya Usimamizi wa Mifumo ya Kifedha na huduma za ndani, Wizara ya Fedha, walitoa maelezo kuhusu matumizi ya Mfumo wa PSPIS na namna ulivyounganishwa na Mfumo wa Kielektroniki wa Ununuzi wa Umma (NeST) kama mbinu ya kuhakikisha mifumo hii inabadilishana taarifa kwa usahihi.

Kikao kazi hicho kimekuwa chachu ya kuimarisha ushirikiano na kubadilishana uzoefu na maarifa kati ya Tanzania Bara na Zanzibar katika usimamizi wa Kada ya Ununuzi wa Umma na Ugavi, pamoja na matumizi ya mifumo ya kidijitali katika kuboresha utendaji wa Serikali.



 

Chapisha Maoni

0 Maoni