Chifu wa Tatu wa Sanjo,
Chifu Faustine Makwai, amesema Tamasha la Sanjo ya Busiya ni nyenzo
muhimu ya utamaduni inayosisitiza upendo na kuwa wamoja.
Aidha
amewataka wananchi kuendeleza mila na desturi zao pamoja na kudumisha
amani.
Kauli hiyo ya kihistoria iliambatana na milio ya ngoma
katika Kata ya Ukenyenge wilayani Kishapu mkoani Shinyanga, ambapo
tamasha hilo la 16 liligeuka daraja la kipekee lililowaleta pamoja
wananchi na machifu kutoka ndani na nje ya nchi, zikiwemo nchi za
Kenya na Afrika Kusini, waliojitokeza kushuhudia na kuenzi urithi huo
mwanana wa Kiafrika.
Mshikamano huo wa kitamaduni ulikolezwa
na Mkuu wa Wilaya ya Kishapu, Peter Masindi, aliyemwakilisha Mkuu wa
Mkoa wa Shinyanga, Mboni Mhita, ambapo alipongeza jinsi sherehe hizo
zilivyowaunganisha Watanzania kusherehekea siku ya Sabasaba kwa amani
na kudhihirisha kuwa wao ni damu moja wanaopaswa kushirikiana katika
kazi na maendeleo.
Wakazi wa Kishapu, akiwemo Bugali Mbushi,
waligubikwa na tabasamu huku wakikiri kuwa tamasha hilo limewajenga
kuwa wamoja na kuwapa nguvu mpya ya kulinda na kuendeleza utamaduni
wao usipotee.

0 Maoni