Waziri
wa Vijana, Joel Nanauka, amewahimiza vijana nchini kujiunga na mifumo
rasmi ya kiuchumi kupitia vikundi, Saccos, vyama vya ushirika na
biashara zilizosajiliwa ili kujiongezea fursa za kiuchumi na
kuboresha maisha yao.
Nanauka alitoa wito huo wakati wa
uzinduzi wa tawi la Benki ya Coop Morocco jijini Dar es Salaam,
akisema ushiriki wa vijana katika mifumo rasmi ya kifedha utawasaidia
kujenga historia nzuri ya kifedha, kupata masoko ya bidhaa na huduma
pamoja na kuimarisha biashara zao.
Amesema hatua hiyo pia
itawawezesha vijana kukidhi vigezo vya kupata mikopo na huduma
nyingine zinazotolewa na taasisi mbalimbali za kifedha, huku
akisisitiza umuhimu wa kuendelea kutoa elimu ya fedha kwa kundi
hilo.
Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa Benki ya Coop,
Godfrey Ng'urah, amesema dhamira ya benki hiyo ni kutatua changamoto
ya upatikanaji wa fedha kwa wananchi wengi kupitia kukuza ujumuishi
wa kifedha.
Ng'urah amesema benki hiyo itaendelea kusogeza
huduma zake karibu na wananchi ili kuwawezesha kupata huduma za
kifedha kwa urahisi zaidi na hivyo kuchochea maendeleo ya
kiuchumi.
Naye Mwenyekiti wa Tume ya Maendeleo ya Ushirika
(TCDC), Abdulmajid Nsekela, amesema lengo la sekta ya ushirika ni
kuhakikisha huduma za kifedha zinawafikia watu wengi zaidi na kuwapa
fursa ya kushiriki kikamilifu katika shughuli za uzalishaji na
maendeleo.

0 Maoni