Taasisi za Madini zaeleza mafanikio robo ya kwanza 2025/26

 

Menejimenti ya Wizara ya Madini Oktoba 27, 2025 ilikutana na Wakuu wa Taasisi zake katika kikao kilicholenga kupokea taarifa ya ufuatiliaji na tathmini kwa majukumu yaliyotekelezwa na taasisi hizo katika kipindi cha Robo ya Kwanza ya Mwaka wa Fedha 2025/26.

Taasisi zilizo chini ya Wizara ni pamoja na Taasisi ya Jiolojia na Utafiti wa Madini Tanzania (GST) Shirika la Madini la Taifa (STAMICO), Tume ya Madini, Taasisi ya Uhamasishaji Uwazi na Uwajibikaji katika Rasilimali Madini, Mafuta na Gesi Asilia (TEITI) na Kituo cha Jemolojia Tanzania (TGC) cha jijini Arusha.

 Katika taarifa iliyowasilishwa na Tume ya Madini, ilielezwa kwamba, katika kipindi robo ya kwanza, tayari kiasi cha shilingi bilioni 315.4 kimekusanywa ikiwa ni sawa na asilimia 105.14 ya lengo la kukusanya shilingi 299.98 bilioni katika robo hiyo. Katika mwaka wa fedha 2025/26 Wizara imepangiwa kukusanya shilingi trilioni 1.4.

Kwa upande wa STAMICO,  pamoja na mambo mengine, taarifa ilieleza kuwa, zoezi la kusimika mitambo ya uzalishaji wa mkaa wa Rafiki Briquettes  unaotokana na makaa ya mawe unaozalishwa na shirika hilo  hivi karibuni itasimikwa katika mikoa ya Dodoma na Tabora. Tayari mitambo kama hiyo inaendelea na uzalishaji  wa nishati hiyo jijini  Dar es Salaam katika eneo la Kisarawe, Pwani na Kiwira mkoani Songwe.

 Aidha,  shirika hilo, lilisistiza kuhusu azma yake  ya kuendeleza leseni zake za madini muhimu na mkakati zilizopo katika maeneo mbalimbali nchini ikiwa ni hatua ya kulifanya kuingia katika uwekezaji mkubwa.

Vilevile, ilielezwa kuwa, katika robo ya kwanza ya mwaka 2025/26 jumla ya kilo 2,356.413 zimesafishwa katika Kiwanda cha Kusafisha Dhahabu cha Mwanza Precious Metals Refinery chenye ubia na STAMICO kwa ajili ya Banki Kuu ya Tanzania. Ilielezwa kwamba, hadi sasa kiasi cha tani 12 za dhahabu tayari zimenunuliwa na benki hiyo kama amana kwa taifa tangu ilipoanza ununuzi rasmi wa dhahabu mwezi Oktoba, 2024.

Pia, pamoja na masuala mengine yaliyojadiliwa, taarifa ya GST kuhusu ununuzi wa helkopita kwa ajili ya shughuli za utafiti wa kina wa madini nchini, ililezwa kwamba, taratibu za manunuzi zinaendelea. Katika bajeti yake ya mwaka 2025/26, Wizara kupitia GST iliahidi kununua helkopita ikiwa ni juhudi za kuhakikisha ifikapo mwaka 2030 angalau asilimia 50 ya nchi iwe imefanyiwa utafiti wa kina. Aidha, GST imeanza ujenzi wa maabara kubwa nchini na ya kisasa Mkoani Dodoma na  kwa ajili ya upimaji wa sampuli mbalimbali nchini. Mara maabara hiyo itakapokamilika italeta ufanisi mkubwa katika shughuli za upimaji sampuli.

Kwa upande wa Kituo cha Jemolojia Tanzania (TGC) pamoja na juhudi zinazoendelea za kukiimarisha kituo hicho kwa kujengwa miundombinu ya majengo, taarifa ya kituo ilileza kwamba, kimefungua duka maalum la kuuza bidhaa za mapambo ya vito na usonara katika eneo la Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha AICC, jijini Arusha. Hivyo kufanya idadi ya maduka hayo kuwa mawili, ukijumuisha na duka lililopo uwanja wa Ndege wa Kimataifa Kilimanjaro ( KIA).


          #Vision 2030: Madini ni Maisha na Utajiri

Chapisha Maoni

0 Maoni