Makwati ahimiza ujirani mwema ili kuimarisha uhifadhi

 

Naibu Kamishna wa Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro (NCAA) anayesimamia Uhifadhi, Utalii na Maendeleo ya Jamii, Joas Makwati, ameongoza kikao cha ujirani mwema na viongozi wa vijiji vinavyopakana na hifadhi hiyo, ambapo amesisitiza umuhimu wa ushirikiano baina ya pande hizo mbili ili kujenga mazingira bora ya kazi na kuimarisha uhifadhi.

Kikao hicho kilichofanyika Oktoba 1, 2025, kiliwahusisha viongozi wa vijiji kutoka wilaya za Karatu na Monduli, na kuhudhuriwa pia na Kamishna Msaidizi Mwandamizi anayeshughulikia Maendeleo ya Jamii kutoka NCAA, Bi. Gloria Bideberi, pamoja na maafisa wengine wa mamlaka hiyo, walikubaliana kufanya kazi kwa pamoja.

Katika mazungumzo yao, viongozi wa vijiji wa wilaya ya Karatu na Monduli waliainisha changamoto zinazowakumba wananchi, kubwa ikiwa ni uvamizi wa wanyama pori kama tembo na nyati katika makazi na mashamba ya wananchi, hali ambayo imesababisha uharibifu mkubwa wa mazao na kutishia ustawi wa kaya zinazotegemea kilimo.

Akizungumza wakati wa kikao hicho, Naibu Kamishna Makwati alieleza kuwa mbali na lengo la kukuza ujirani mwema, majadiliano hayo yameweka msingi wa mipango ya pamoja ya kutatua changamoto kati ya binadamu na wanyama pori.

Kwa mujibu wa NCAA, mamlaka hiyo itaendelea na ziara katika vijiji mbalimbali vinavyozunguka hifadhi, kwa lengo la kuimarisha mahusiano na kuwashirikisha wananchi katika shughuli za uhifadhi na maendeleo ya jamii.



Chapisha Maoni

0 Maoni