Dkt. Samia aahidi kurejesha uhai wa zao la chai Mufindi

 

Mgombea urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia Chama cha Mapinduzi (CCM), Dkt. Samia Suluhu Hassan, ameahidi kulifufua zao la chai wilayani Mufindi, mkoani Iringa, ikiwa ni pamoja na kuhakikisha mashamba yaliyotelekezwa na wawekezaji binafsi yanarudishwa kwa vyama vya ushirika.

Akizungumza leo Septemba 6, 2025, katika mkutano wa kampeni uliofanyika Nyororo, Dkt. Samia alisema tayari Serikali imeunda timu maalum ya kufanya tathmini ya hali ya uwekezaji katika sekta ya chai nchini, ili kuchukua hatua madhubuti za kulinda maslahi ya wakulima.

“Tumeamua kuwa mashamba ambayo hayajaendelezwa na wawekezaji, yarudi kwa wananchi kupitia vyama vya ushirika. Tunataka zao la chai lirudi kuwa chanzo kikuu cha mapato kwa Mufindi na maeneo mengine ya Nyanda za Juu Kusini,” alisema Dkt. Samia.

Wafanyakazi wa Kampuni ya Chai Kulipwa

Katika hatua nyingine, Dkt. Samia aligusia malalamiko ya wafanyakazi wa Kampuni ya Chai na Kahawa ya Mufindi (Mufindi Tea and Coffee Company) ambao wanadai zaidi ya Sh bilioni 2.7. Alisema Serikali inaratibu mazungumzo na pande husika ili kuhakikisha wafanyakazi hao wanalipwa haki zao stahiki.

“Tumeshapokea taarifa rasmi juu ya madai ya wafanyakazi wa kampuni hiyo. Mazungumzo yanaendelea, na Serikali itahakikisha stahiki zao zinalipwa,” alieleza.

Barabara za Lami, X-ray na Huduma za Afya

Dkt. Samia pia alitangaza kuendelea kwa miradi ya miundombinu, ikiwemo ujenzi wa barabara ya lami ya Nyororo–Mtwango yenye urefu wa kilomita 40.4 na Igowole–Kasanga–Nyigo yenye kilomita 54.5.

Aidha, aliahidi kupeleka mashine ya X-ray katika Hospitali ya Wilaya ya Mufindi ili kuboresha huduma za uchunguzi wa kiafya kwa wananchi wa wilaya hiyo.



Chapisha Maoni

0 Maoni