Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC) leo Jumatano
imetangaza rasmi majina ya wagombea wa nafasi ya Urais wa Jamhuri ya Muungano
wa Tanzania kwa Uchaguzi Mkuu unaotarajiwa kufanyika Oktoba 29, 2025.
Akizungumza katika hafla maalum iliyofanyika katika ofisi za
INEC jijini Dodoma, Mkurugenzi wa Uchaguzi, Ramadhan Kailima, alithibitisha
kuwa wagombea wote waliotimiza masharti ya kikatiba na kisheria wameteuliwa
rasmi kuingia kwenye kinyang’anyiro hicho kikuu cha kisiasa nchini.
Katika hatua ya kipekee mwaka huu, INEC imeanza utekelezaji
wa utaratibu mpya wa kuwapatia wagombea magari mapya pamoja na dereva na mlinzi
mara baada ya uteuzi wao kuthibitishwa.
Wagombea wote walikabidhiwa magari mapya aina ya Toyota Land
Cruiser GXR, ambapo Kailima alieleza kuwa hatua hiyo inalenga kuhakikisha
usalama na usawa katika shughuli za kampeni.
“Utaratibu huu umewekwa kisheria. Mgombea anapokidhi vigezo
vya kuteuliwa, INEC inawajibika kumkabidhi gari jipya, pamoja na dereva na
mlinzi, kwa ajili ya shughuli za kampeni,” alisema Kailima.
INEC imeeleza kuwa hatua hiyo ni sehemu ya maboresho ya mchakato
wa uchaguzi, yanayolenga kuweka mazingira bora na salama kwa wagombea wote,
bila kujali uwezo wao wa kifedha au rasilimali.
0 Maoni