Mlipuko wa volkano wasitisha safari za ndege Indonesia

 

Mlima wa volkano wa Lewotobi Laki Laki uliopo katikati mwa Indonesia ulilipuka Jumanne jioni na kutema wingu kubwa la majivu moto hadi umbali wa kilomita 11 juu ya anga, hali iliyosababisha usumbufu mkubwa wa safari za ndege kuelekea na kutoka kisiwa maarufu cha utalii cha Bali.

Kwa mujibu wa taarifa ya Wakala wa Jiolojia wa nchi hiyo, mlipuko huo ulitokea saa 11:35 jioni kwa saa za huko, ambapo moshi wenye umbo la uyoga wa rangi ya machungwa ulifunika kijiji cha Talibura kilichopo karibu na mlima huo, huku mashuhuda wakiripoti kuuona moshi huo hadi umbali wa kilomita 150.

Mamlaka za Indonesia zimetangaza hali ya tahadhari ya juu kabisa na kuwaonya watalii na wakazi kukaa mbali na eneo hilo kwa sababu za kiusalama.

Kutokana na tukio hilo, safari kadhaa za ndege zimesitishwa katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Denpasar, Bali. Tovuti ya uwanja huo imeeleza kuwa sababu ya usumbufu huo ni "kutokana na mlipuko wa volkano".

Safari zilizohusika ni pamoja na zile za ndani kuelekea Jakarta na Lombok, pamoja na za kimataifa kwenda nchi za Australia, China, India, Malaysia, New Zealand na Singapore.

Mamlaka zinaendelea kufuatilia hali hiyo kwa karibu huku juhudi za kuwaokoa watu walioko katika maeneo hatarishi zikiendelea.

Chapisha Maoni

0 Maoni