Waziri ajiuzulu Japan kisa utani kuhusu mchele

 

Waziri wa Kilimo wa Japan Taku Eto amejikuta akilazimika kujiuzulu wadhifa wake baada ya kuongelea kwa mzaha tatizo la kupanda kwa bei ya mchele nchini humo.

Waziri  huyo alipotangaza kuwa hajawahi kununua mchele kwa sababu wafuasi wake humpa "wa kutosha" kama zawadi, alitarajia kuchekesha tu. Lakini mdomo ulikiponza kichwa.

Japan inakumbwa na mgogoro wa gharama ya maisha kwa mara ya kwanza baada ya miongo kadhaa, na hili limeathiri chakula pendwa sana cha mchele.

Bei ya mchele imepanda maradufu Japan katika kipindi cha mwaka mmoja uliopita, na aina zinazoagizwa kutoka nje ni chache sana.

Eto ameomba radhi, akisema kuwa alipinduka mipaka kwa kauli yake aliyotoa Jumapili katika shughuli ya kuchangisha fedha huko nyumbani kwao.

Waziri Eto alijiuzulu baada ya vyama vya upinzani kutishia kuwasilisha hoja ya kutokuwa na imani naye.

Kuondoka kwake kunaleta pigo jipya kwa serikali ya wachache inayoongozwa na Waziri Mkuu Shigeru Ishiba, ambayo tayari ilikuwa inakumbwa na kuporomoka kwa uungwaji mkono wa umma.



Chapisha Maoni

0 Maoni