DC Masasi awatembelea majeruhi wa ajali ya bus la abiria Masasi

 

Mkuu wa Wilaya ya Masasi Mhe. Rachel Kassanda amewajulia hali majeruhi wa ajali ya Bus la abiria aina ya Maning Nice lenye namba za usajili T 848 ELA iliyotokea alfajiri ya jana Mei 7, 2025 katika eneo la Sululu Wilaya ya Masasi mkoani Mtwara.

Akizungumza mara baada ya kuwaona majeruhi amesema ajali hiyo imetokea alfajiri ya kuamkia leo ambapo bus hilo lilikuwa linatokea Dar es Salaam kuelekea Tunduru na kwamba hakuna kifo kilichotokea na kuna majeruhi 23 ambao wapo  Hospitali ya Mkomaindo na baadhi yao wamepewa rufaa ya kwenda Hospitali ya Rufaa Ndanda.

“Hongereni madaktari hatua ambazo mmezichukua zinatia moyo, endeleni kupambana ili wote waruhusiwe salama waweze kuendelea na shughuli zao,” amesema Mhe. Kassanda.

Mhe. Kassanda ametoa rai kwa wamiliki wa mabus kuhakikisha wanakuwa na madereva wawili kwa nyakati za usiku ili kuepusha ajali zinazotokana na uchovu wa madereva.

Aidha, ameliagiza Jeshi la Polisi Wilaya ya Masasi kufanya ukaguzi wa mara kwa mara wa kuhakikisha madereva wote wawili wanakuwepo kwenye mabus yanayosafiri nyakati za usiku ili kuleta ufanisi wa safari na usalama wa abiria.

Mganga Mkuu wa Halmashauri ya Mji Masasi Dkt. Salum Gembe amesema hakuna kifo kilichotokea katika ajali hiyo na majeruhi wote wanaendelea kupata matibabu katika Hospitali ya Mkomaindo.

“Tumepokea majuruhi 23, watoto 3 wa kiume, wanawake 9, wanaume 11 ambao wameumia sehemu mbalimbali za mwili lakini Mungu amesaidia hakuna kifo hata kimoja, wote wanaendelea na matibabu hapa Mkomaindo, mmoja tu tumempa rufaa ya kwenda Ndanda Hospitali,” amesema Dkt. Gembe.



Chapisha Maoni

0 Maoni