Menejimenti
ya Shirika la Hifadhi za Taifa Tanzania (TANAPA) inayoongozwa na Kamishna wa
Uhifadhi, Juma Nassoro Kuji, imeweka vipaumbele muhimu katika bajeti mpya ya
mwaka wa fedha 2025/2026 ili kuboresha shughuli za uhifadhi na utalii.
Vipaumbele
hivyo vimewekwa katika kikao kazi cha Menejimenti ya Shirika kilicholenga
kujadili maandalizi ya mwisho ya bajeti ya Shirika kwa mwaka mpya wa fedha wa
2025/2026. Kikao hicho kimefanyika jana Aprili 04, 2025 katika ukumbi wa
mikutano uliopo Hifadhi ya Taifa Manyara.
Akizungumza
na washiriki wa kikao, Kamishna Kuji alieleza dhima ya Shirika katika
kutengeneza bajeti inayoangazia vipaumbele vinavyotatua changamoto na kuboresha
utendaji na utekelezaji wa majukumu ili kufikia malengo ya Shirika na Taifa kwa
ujumla.
“Mwaka ujao
wa fedha wa 2025/2026 tunaweka mkazo katika kuongeza nguvu kwenye shughuli za
ulinzi na usalama wa hifadhi, kuendelea kuboresha miundombinu ya utalii,
kuboresha upatikanaji na uboreshaji wa vitendea kazi kama vile kupata magari
kwa ajili ya doria na kukarabati magari yenye uhitaji huo.” alisema Kamishna
Kuji.
Pia, Kamishna
Kuji alisisitiza kutengeneza bajeti itakayolenga kutoa msukumo katika
uanzishaji wa mazao mapya ya utalii ili kuongeza mapato ya Shirika na Taifa,
ushirikishwaji wa jamii katika shughuli za uhifadhi, matumizi ya teknolojia,
utatuzi wa migogoro kati ya wanyamapori wakali na waharibifu na binadamu
sanjali na kuboresha maslahi kwa
watumishi.
Wajumbe wa
kamati ya bajeti ya Shirika wilipata fursa ya kuwasilisha taarifa ya
utekelezaji wa bajeti ya Shirika inayoendelea ya mwaka 2024/2025 ambapo walibainisha maeneo ya
msingi ambayo yametekelezwa kwa ufanisi ikiwemo kuhamasisha watanzania
kuchangamkia fursa ya kufanya utalii wa ndani kwa kutembelea Hifadhi za Taifa
na Vituo vya Malikale vilivyokasimishwa kwa TANAPA.
Sambamba na
hilo pia, Kamati ilieleza maeneo mengine
ya kuweka kipaumbele ni pamoja na kuendelea kufanya maboresho ya miundombinu ya
utalii na utawala ikiwemo matengenezo ya barabara zilizopo hifadhini, ujenzi wa
malango ya utalii na ujenzi wa hosteli zinazotumiwa na wanafunzi wanapotembelea
Hifadhi za Taifa, udhibiti wa mimea vamizi, udhibiti wa wanyamapori wakali na
waharibifu, utoaji wa elimu ya uhifadhi kwa jamii na utekelezaji wa miradi
mingine ya maendeleo.
Naye, Kamishna
Msaidizi Mwandamizi wa Uhifadhi, Sekela Mwangota, ambaye ndie Katibu wa Kamati
ya Bajeti ya Shirika alielezea namna bajeti mpya ilivyoandaliwa.
“Uandaaji wa
mapendekezo ya bajeti ya Shirika kwa mwaka wa fedha 2025/2026 umezingatia Ilani
ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi (CCM) ya mwaka 2020, Mwongozo wa Maandalizi
ya Mpango na Bajeti ya Serikali wa Mwaka 2025/2026, Mpango Mkakati wa Shirika,
Sheria, Kanuni na Taratibu mbalimbali za nchi, vipaumbele vya Shirika na Nchi
pamoja na maelekezo mahsusi ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
yanayolenga kuboresha ustawi wa jamii ya watanzania” alieleza Kamishna Sekela.
Mapendekezo
ya Bajeti ya Shirika kwa mwaka wa fedha 2025/2026 yatawasilishwa katika ngazi
mbalimbali za maamuzi kwa ajili ya uchambuzi na idhini kabla ya kuanza kutumika
rasmi mnamo tarehe 01.07.2025.
Shirika
linaendelea kutekeleza majukumu yake ili
kuhakikisha kuwa uhifadhi endelevu wa maeneo yote yaliyotengwa kuwa
hifadhi za Taifa nchini unaimarika kwa ajili ya manufaa ya kizazi cha sasa
na vizazi vijavyo.
Na. Andrew
Mbai - Mto wa Mbu



0 Maoni