NEC CCM Yapongeza Tume ya Jaji Chande

 

KATIBU wa Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC) Itikadi, Uenezi na Mafunzo wa Chama Cha Mapinduzi, Kenani Laban Kihongosi amesema Halmashauri Kuu ya CCM ya Taifa (HKT) imefanya kikao chake cha kawaida jijini Dodoma chini ya Mwenyekiti wake, Dkt. Samia Suluhu Hassan ambaye pia ni Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Kwa mujibu wa taarifa hiyo ya Kihongosi iliyotolewa leo Alhamisi Mei 7, 2026, pamoja na mambo mengine Halmashauri Kuu ilifanya tathmini ya Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2025 na kujadili hali ya kisiasa nchini.

Amesema katika kikao hicho, Halmashauri Kuu ya CCM ya Taifa ilimshukuru na kumpongeza Mwenyekiti wa CCM na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kuunda Tume ya Rais ya kuchunguza matukio yaliyotokea wakati na baada ya Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 2025.

Pia, Halmashauri Kuu imeipongeza Tume ya Uchunguzi iliyoongozwa na Jaji Mkuu Mstaafu Mohamed Chande Othman kwa kufanya kazi yake kwa weledi, uadilifu na kwa kuzingatia misingi ya sheria za nchi na za kimataifa. Aidha, imeipongeza Serikali kwa hatua zilizoanza na zitakazoendelea kuchukuliwa katika kutekeleza mapendekezo yote yaliyotolewa na tume hiyo.

Katika hatua nyingine, Halmashauri Kuu kwa kauli moja imevipongeza vyombo vya ulinzi na usalama kwa kazi kubwa ya kulinda nchi na kuhakikisha hali ya amani na utulivu inarejea haraka katika maeneo yote ya nchi mara baada ya Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2025.

Vilevile, kikao hicho kimeunga mkono pendekezo la Kamati Kuu kutoka kikao chake cha Aprili 28 hadi 29, 2026 la kufanya tathmini ya kina ya CCM kwa lengo la kukiimarisha na kuchukua hatua thabiti za kukiboresha kimuundo, kiutendaji na kiuchumi.

#MezaYaUmoja

Chapisha Maoni

0 Maoni