Muhimbili Mloganzila yahitimisha kambi maalum ya upandikizaji figo

 

Hospitali ya Taifa Muhimbili Mloganzila imehitimisha kambi ya upasuaji wa upandikizaji figo kwa kuwapandikiza wagonjwa watano ambapo figo imevunwa kutoka kwa wachangiaji kwa kutumia njia ya kisasa ya matundu (Hand Assisted Laporascopic Donor Nephrectomy).

Kwa mujibu wa Bingwa wa Magonjwa ya Figo, Dkt. Immaculate Goima kambi hiyo iliyochukua takribani siku tatu kuanzia Januari 29 hadi 31, 2025 imehusisha wataalam wa ndani ambao wameshirikiana na wataalam kutoka Korea Kusini.

Dkt. Goima amesema kutokana na utaalam uliotumika kuvuna figo kutoka kwa wachangiaji imewafanya wachangiaji hao kukaa hospitalini kwa muda mfupi ambapo watakaa wodini kati ya siku mbili hadi tatu na kuruhusiwa kurejea nyumbani kwao kuungana na familia zao.

Dkt. Goima ameongeza kuwa kutokana na uwekezaji uliofanywa na Serikali wa kusomesha wataalam, kununua vifaa tiba, vitendanishi na kujenga uhusiano mzuri na mataifa mbalimbali duniani kumesaidia kutoa huduma hizi za ubingwa bobezi hapa nchini kwa weledi na ubora wa hali ya juu.

Hospitali ya Taifa Muhimbili Mloganzila ndio hospitali pekee hapa nchini inayotumia utaalam wa kuvuna figo kutoka kwa mchangiaji kwa kutumia njia ya matundu madogo, baada ya upandikizaji huo hospitali hiyo inafikisha idadi ya wagonjwa 16 waliopandikiza figo tangu huduma hiyo ilipoanza kutolewa Muhimbili Mloganzila Aprili, 2023.



Chapisha Maoni

0 Maoni