Jeshi la Uhifadhi msihifadhi maliasili peke yake - Mhe. Kitandula

 

Maafisa na Askari wa Jeshi la Uhifadhi walioko kwenye maeneo yenye Mradi wa Kuboresha Usimamizi wa Maliasili na Kukuza Utalii Kusini mwa Tanzania (REGROW) wametakiwa kutokuhifadhi maliasili peke yake bali na miundombinu inayoendelea kuboreshwa kwenye hifadhi za Taifa.

Wito  huo umetolewa na Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Mheshimiwa Dunstan Kitandula alipokuwa akiongea na viongozi wa Kanda ya Kusini  na hifadhi ya Taifa Ruaha alipokuwa katika ziara ya kukagua miradi inayojengwa chini ya ufadhili wa mradi wa Kuboresha Usimamizi wa Maliasili na Kukuza Utalii Kusini mwa Tanzania (REGROW).

Mhe. Kitandula alisema kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan amefanya jitahada kubwa za kutangaza sekta ya utalii kupitia Filamu za Tanzania The Royal Tour na Amazing Tanzania ili kuongeza idadi ya watalii, hivyo kama wahifadhi hatuna budi kutimiza wajibu wa uhifadhi wa maliasili na vivutio vya utalii vilivyopo ikiwemo kuhifadhi miundombinu inayojengwa katika hifadhi mnazozisimamia.

Aidha, Mhe. Kitandula hakusita kuwaonya na kuwakumbusha watumishi wanaofanya kazi katika kampuni zilizopata kandarasi ya kujenga miundombinu hiyo kuwa wanatakiwa kuwa wazalendo kwa kuhakikisha miradi hiyo inajengwa kwa kufuata mikataba iliyowekwa na kutokujengwa chini ya viwango kwa kuwa miradi hii ni ya watanzania wote.

Mradi wa REGROW umefadhili ujenzi wa majengo mbalimbali katika Hifadhi ya Taifa Ruaha ikiwemo uboreshaji wa viwanja viwili vya Ndege, kujenga jengo la ikolojia, hostel kwa ajili ya makundi makubwa ya watalii na kuinua wananchi mbalimbali kiuchumi kupitia vikundi vya COCOBA na kusaidia wananchi wanaoshi kando ya hifadhi ya Ruaha kukabiliana na Changamoto ya Wanyama wakali na waharibifu.


   Anangisye Mwateba - Hifadhi ya Taifa Ruaha

Chapisha Maoni

0 Maoni