Kamishna Kuji abainisha chanzo cha mafanikio ya TANAPA

Kamishna wa Uhifadhi TANAPA, Musa Nassoro Kuji amebainisha kuwa mafanikio yanayopatikana katika Shirika la Hifadhi za Taifa Tanzania (TANAPA) ni matokeo ya nidhamu, bidii, na uadilifu miongoni mwa Maafisa na Askari wa Uhifadhi katika kutekeleza majukumu ya Shirika.

Kamishna Kuji, ameyasema hayo katika ziara yake ya kikazi aliyoifanya jana tarehe 12.11.2024 katika Hifadhi ya Taifa Ziwa Manyara ikiwa na lengo la kuzungumza na Maafisa na Askari hao waliopo katika hifadhi hiyo.

“Nitoe pongezi zangu kwa mafanikio ambayo Shirika limeyafikia kupitia hifadhi zake ambapo Ziwa Manyara ni mojawapo ya hifadhi hizo. Mpaka sasa Shirika limekusanya zaidi ya asilimia 75 ya bajeti ya mwaka, kwani matarajio yetu mwaka huu ni kukusanya trillioni na kuondoka kwenye mabillioni. Haya yote ni matokeo ya uadilifu, nidhamu na kujituma kwa kila mmoja wetu katika kutekeleza majukumu yetu.”

“Hii ni kazi kubwa mnayoifanya na ndio kazi tuliyotumwa na Amiri Jeshi Mkuu, Mhe. Dkt.Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Kutii mamlaka ni mwanzo wa kufungua baraka hivyo nisisitize nidhamu na uadilifu zaidi katika kutekeleza majukumu ya Shirika.”

Akiwasilisha taarifa ya hifadhi, Kamishna Msaidizi wa Uhifadhi, Dkt. Yustina Kiwango ambaye ni Mkuu wa Hifadhi ya Taifa Ziwa Manyara alimpongeza Kamishna wa Uhifadhi kwa kutenga muda wake na kwenda kuwatembelea na kusikiliza changamoto za hifadhi, Askari na Maafisa wa Jeshi la Uhifadhi waliopo katika hifadhi hiyo. Pia, ameipongeza Bodi ya Wadhamini TANAPA pamoja na Menejimeti ya Shirika kwa kuwezesha ufunguzi wa maeneo ya hifadhi ambayo kwa kiasi kikubwa yaliathiriwa na mabadiliko ya tabia nchi pamoja na kuondoa mimea vamizi.

“Niishukuru Bodi ya Wadhamini, pamoja na Menejimenti ya Shirika kwa mchango mkubwa mnaotupatia sisi Hifadhi ya Taifa Ziwa Manyara ambapo tumeweza kufungua maeneo ya hifadhi zaidi ya ekari 400, na kwa sasa watalii wanafurahia kuona ufunguzi wa maeneo haya ambayo yaliathirika na mabadiliko ya tabia nchi ambapo maji ya ziwa yalimeza maeneo ya malisho ya wanyama na kupelekea kuwa na wanyama wachache wanaooneka na uwepo wa vichaka vingi,”alisema Kamishna Kiwango.

Hifadhi ya Taifa Ziwa Manyara imefanikiwa kufungua maeneo mbalimbali kwa kiwango cha changarawe ikiwemo eneo la njia panda ya Wayo hadi daraja la Endabashi, eneo la geti la Mahogan, Majimoto hadi Mto Array, eneo la Migunga ya Nyani, pamoja na Barabara ya kutoka kituo cha Daudi hadi ATM. Maeneo hayo ya hifadhi ni miongoni mwa maeneo yaliyoathiriwa kwa kwa kiasi kikubwa na mabadiliko ya tabia nchi.

   Na. Edmund Salaho- Ziwa Manyara

Chapisha Maoni

0 Maoni