Hatifungani ya Miundombinu ya Barabara neema kwa Makandarasi

 

Imeelezwa kuwa uanzishwaji wa Hatifungani ya Miundombinu ya Barabara (Samia Infrastructure Bond) unaenda kuondoa changamoto ya ucheleweshaji wa malipo ya Makandarasi kwa wakati wanapokuwa wamekamilisha kazi.

Hayo yameelezwa jana Novemba 29 na Mtendaji Mkuu wa Wakala ya Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA), Mhandisi Victor Seff wakati akitoa taarifa fupi katika hafla ya uzinduzi wa Hatifungani ya Miundombinu ya Barabara za Wilaya (Samia Infrastructure Bond) mbele ya Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Philip Isdory Mpango ambaye alimwakilisha Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Aidha, Mhandisi Seff amebainisha kuwa kuanzishwa kwa Hatifungani hiyo ni muendelezo wa utatuzi wa changamoto wanazokabiliana nazo wakati wa utekelezaji wa jukumu la usimamizi, ujenzi na matengenezo ya miundombinu ya barabara za wilaya zenye urefu wa Kilomita 144,429.77 ikiwa ni pamoja na madaraja 3,560 pamoja na makalavati 80,326.

"Changamoto kubwa tuliyo nayo katika utekelezaji wa jukumu letu ni pamoja na ufinyu wa bajeti lakini pia uchelewashaji wa malipo ya Makandarasi wanapokuwa wamekamilisha kazi na hivyo kushindwa kuwalipa kwa wakati kulingana na mikataba."

"Uanziwashwaji wa Hatifungani hii unaenda kuondoa changamoto hii pamoja na utoaji wa dhamana za malipo ya awali na utendaji wa Makandarasi na Wahandisi Washauri/Wasimamizi," alifafanua Mhandisi Seff.

Hata hivyo, Mhandisi Seff alieleza kuwa uanzishwaji wa Hatifungani hiyo ni utekelezaji wa maagizo ya Rais Samia Suluhu Hassan aliyowaasa na kuwashauri TARURA kuwa wabunifu na kufikiri nje ya boksi ili kukabiliana na changamoto ikiwemo matumizi ya malighafi zinazopatikana maeneo ya kazi na matumizi ya teknolojia mbadala kwa lengo la kupunguza muda wa utekelezaji na kutunza mazingira.

Kuhusu ubunifu, Mhandisi Seff ameongeza kuwa hadi sasa wameweza kujenga jumla ya madaraja 350 na kilomita 29 za barabara kwa kutumia mawe ambapo gharama zimepungua kutoka Bilioni 97 hadi Bilioni 30 sawa na asilimia 60.



Chapisha Maoni

0 Maoni