186 waonwa kambi maalum ya matibabu ya maumivu makali Muhimbili

 

Wananchi 186 wenye maumivu makali wamejitokeza Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH) kwenye kambi maalum inayoendelea ambapo 25 kati yao tayari wametibiwa kupitia tiba radiolojia na kuondokana na changamoto hiyo kupitia sindano za; goti, uti wa mgongo kwenye pingili za uti wa mgongo, sindano za kuua neva zinazo husiana na maumivu ya nyonga au mabega pamoja na matibabu ya maumivu ya tumbo yasababishwayo na saratani ya kongosho.

Akizungumza na vyombo vya habari leo Jijini Dar es Salaam, Mkurugenzi Mtendaji wa MNH Prof. Mohamed Janabi amesema maumivu makali yanasababishwa na mambo kadhaa ikiwemo kudhoofika kwa viungo vya mwili kutokana na umri, saratani, kusagika kwa diski za pingili za mgongo , majeraha yaliyotokea muda mrefu uliopita n.k

Prof. Janabi amesema kambi hiyo si tu imewanufaisha wagonjwa, pia imetumika kama jukwaa la kipekee la kuhamisha ujuzi kwenda kwa wataalam wazalendo ambao wataendelea kutoa matibabu hayo hatua kwa hatua na kuifanya huduma hiyo kuwa endelevu hapa nchini.

Kwa upande wake Prof. David Prologo, Bingwa Mbobezi kutoka Hospitali ya Emory Johns Creek ya nchini Marekani aliyeongoza timu ya madaktari wabobezi, idara ya radiolojia MNH, kitengo cha tiba radiolojia amesema anajivunia utalaam uliopo hususani vifaa tiba vya kisasa na watalaam wabobezi ambao wameshirikiana kutoa huduma hiyo.

Prof. Prologo amekiri uwepo wa umahiri wa wataalam wa ndani wa kutoa matibabu hayo kwa uendelevu wa huduma hiyo hata asipokuwepo.

Akihitimisha mkutano huo, Prof. Janabi amemshukuru Prof. Prologo kwa kujitolea kwake kuboresha huduma za afya katika taifa letu pamoja na taasisi ya Road2IR ambayo siyo tu imechangia kuanzishwa kwa tiba radiolojia nchini bali imeendelea kuratibu safari za wataalam wa tiba radiolojia kutoka sehemu mbalimbali duniani hususani Marekani na Ulaya kuleta ujuzi wao nchini.

Chapisha Maoni

0 Maoni