Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Balozi Dk. Emmanuel John Nchimbi amesema CCM, chini ya uongozi wa Mwenyekiti wake, Ndugu Dk. Samia Suluhu Hassan, itaendelea kutoa uongozi na kusimamia ili kuhakikisha diplomasia ya uchumi na siasa inaendelea kuiwezesha Tanzania na Watanzania wote kwa ujumla, kunufaika na fursa za kiuchumi zinazopatikana ndani na nje ya nchi.
Balozi Dk. Nchimbi amesema mabadiliko mbalimbali ya kisera na
mwelekeo, chini ya Serikali ya CCM, inayoongozwa na Rais Dk. Samia Suluhu
Hassan, yameendelea kuwa sehemu ya dira ya Tanzania katika kutafuta matokeo
chanya ya haraka yanayolenga kuhakikisha Tanzania inakuwa mnufaikaji sawa
katika uhusiano unohusisha pande mbili, kila wakati, iwe kati ya nchi na nchi
au nchi na taasisi za kimataifa.
Katibu Mkuu wa CCM Balozi Dk. Nchimbi ameyasema hayo
alipokutana na kufanya mazungumzo kwa nyakati tofauti na Mabalozi wa Nchi za
Misri na Korea Kaskazini wanaowakilisha nchi zao nchini Tanzania, Mhe. Sherif
Abdelhanid Ismail na Komredi Kim Yong Su, mtawalia, pamoja na Mkurugenzi Mkazi
wa Taasisi ya Friedrich-Ebert-Stiftng (FES), nchini, Bi. Elisabeth Bollrich,
Ijumaa, Aprili 5, 2024, Ofisi Ndogo za Makao Makuu ya CCM, Lumumba, jijini Dar Es Salaam.
Kwa upande wake, Mhe. Balozi Sherif Abdelhanid Ismail
amemhakikishia Balozi Dk. Nchimbi kuwa Nchi ya Misri, chini ya uongozi wa Rais
Abd el-Fattah Saeed Hussein Khalil el-Sisi, inaichukulia Tanzania kuwa
mmojawapo wa washirika wake wa karibu katika nyanja mbalimbali za maendeleo,
ikizingatiwa kuwa nchi hizo mbili zimekuwa na ushirikiano katika miradi mikubwa
yenye athari chanya kwa uchumi wa pande zote mbili.
Naye Balozi Kim Yong Su katika mazungumzo yake na Balozi Dk.
Nchimbi alisema kuwa Nchi ya Korea Kusini, chini ya Rais Kim Jong Un, ambaye
pia ni Katibu Mkuu wa Chama cha Wafanyakazi wa Korea (WPK), kinachoongoza nchi
hiyo, ambacho ni chama rafiki na CCM, siku zote imekuwa tayari kudumisha na
kuenzi urafiki na uhusiano wa nchi hizo mbili na vyama hivyo viwili, uliowekewa
misingi imara tangu wakati wa Kiongozi wa Kwanza wa Korea Kaskazini, Komredi Kim
Il Sung na Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere.
Halikadhalika, Mkurugenzi Mkazi wa Taasisi ya FES, Bi.
Elisabeth Bollrich, pamoja na masuala mengine alimwelezea Balozi Dk. Nchimbi
jinsi ambavyo FES imekuwa ikifanya kazi nchini, ambapo Katibu Mkuu huyo wa CCM
alimhakikishia ushirikiano kwa masuala yenye maslahi kwa Tanzania.
0 Maoni