Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF) limesema limepokea kwa
masikitiko taarifa ya kifo cha Rais Mstaafu wa Awamu ya Pili wa Tanzania, Ali
Hassan Mwinyi aliyefariki dunia jana Februari 29, 2024 katika Hospitali ya
Mzena, Jijini Dar es Salaam alikokuwa anapatiwa matibabu.
Katika salamu hizo Mwenyekiti wa Jukwaa la Wahariri (TEF),
Deodatus Balile amesema Mzee Mwinyi katika uongozi wake alianzisha demokrasia
ya Vyama Vingi vya Siasa Tanzania, aliondoa vikwazo kwa kampuni binafsi,
akapunguza vikwazo vya uagizaji bidhaa kutoka nje, na kupata jina la utani la
“Mzee Ruksa”, msemo wa Kiswahili ambao unaweza kutafsiriwa kama “Ruhusa ya
Mheshimiwa kutenda lililo jema” na kuwafanya Watanzania wajue na kushika fedha
katika uongozi wake.
Ameongeza kuwa, Mzee Mwinyi alisisitiza uwajibikaji kazini na
kukemea wazembe, kwa kuasisi maneno “fagio la chuma” maana wazembe wote walikuwa
wakiondolewa kazini au kupunguzwa kazi. Ndiye aliyeruhus watumishi kujitafutia
kipato cha ziada baada ya saa za kazi madaktari wakaanza kufanya kazi kwenye
vituo vingine na hata kufungua hospitali zao binafsi pia Aliamini katika ukuaji
wa Uchumi kwa mtu mmoja mmoja kwa maendeleo ya familia na taifa.
Pia, Balile amesema Mzee Mwinyi wakati wa uhai wake
alichagiza michezo na yeye alikuwa mpenda michezo hasa jogging (kukimbia). Pia
alikuwa mwandishi wa mashairi na vitabu.
Balile amemalizia kwa kusema kwa pamoja TEF wanaungana na
familia ya Mzee Ali Hassan Mwinyi na Watanzania wote kuomboleza msiba huo
mkubwa kwa taifa.
Mungu ailaze mahala pema peponi roho ya Mzee Mwinyi.
0 Maoni