Mkuu wa Wilaya ya Bunda Mhe. Dkt. Vicent Anney amesema
wananchi wa wilaya yake wananufaika sana na uwepo wa Mamlaka ya Usimamizi wa Wanyamapori Tanzania
- TAWA kutokana na ufadhili wa miradi
mbalimbali ya maendeleo inayotokana na shughuli za uwindaji wa kitalii
unaofanyika katika Pori la Akiba Grumeti.
Dkt. Vicent ameyasema hayo wakati wa ziara
ya kutembelea na kukagua miradi ya maendeleo iliyofadhiliwa na TAWA wilayani
humo.
"Nichukue nafasi hii kuishukuru TAWA kwa uwepo wake
katika wilaya ya Bunda, pia tunaishukuru Serikali kwa mipango yake kwasababu
imetusaidia sisi wananchi wa Bunda kupata huduma mbalimbali za kijamii ambazo
zimetokana na gawio linalotokana na shughuli za uwindaji zinazofanywa katika
maeneo ya Bunda, " amesema Dkt. Vicent.
Mkuu huyo wa wilaya amesema TAWA imefadhili miradi miwili
katika Kata ya Hunyari Kijiji cha Sarakwa ambayo ni darasa moja (1) na Ofisi
moja (1) ya Mwalimu Mkuu, samani za shule ambazo ni jumla ya madawati 100, vitu
vya walimu 12, meza 5 za walimu na mantenki matatu yenye ujazo wa Lita 2000 kwa
ajili ya kuwasaidia wanafunzi kuhifadhi maji pamoja na nyumba mbili (2) za
walimu ambazo zimesaidia kuboresha ufundishaji kwa kuwa walimu wanakuwa na
utulivu wa mawazo.
Wananchi wa kijiji cha Sarakwa wameishukuru Serikali na
kukiri kuwa TAWA ndiyo taasisi pekee iliyojitokeza kufadhili miradi mikubwa
katika Kijiji hicho tangu kuanzisha kwake, baada ya wananchi kuhangaika kwa
muda mrefu kukamilisha miradi hiyo kwa nguvu zao bila mafanikio na hivyo
kukibatiza Kijiji chao kwa jina la "Kijiji cha TAWA".
"Tangu kuanzishwa kwa Kijiji hiki Mwaka 2014, Kijiji
hiki na shule hii (Shule ya Msingi Steven Wasira) haikuwahi kupata mradi
wowote, TAWA pekee ndiyo imekuwa ya kwanza kutoa mradi mkubwa wa madawati 100,
kumalizia chumba cha darasa moja (1), meza 5 na viti 12 vya walimu na ofisi 1
ya walimu kwahiyo Kijiji hiki tunakipa jina TAWA," amesema Mwenyekiti wa
Kijiji Kijiji cha Sarakwa Giragu Gisunu Nyarumuga.
Naye Mwenyekiti wa Kamati ya Shule ya Msingi Steven Wasira
Paulo Kisumda amesema miradi hiyo iliyofadhiliwa na TAWA katika Kijiji cha Sarakwa imesaidia kupunguza
migongano kati ya wananchi na wanyamapori ambapo amekiri kuwa awali walikuwa
wanawachukia Wanyamapori lakini tangu waanze kupata miradi hii wamegundua wanyamapori wana faida kubwa, na wao kama
wananchi ni sehemu ya wamiliki wa
rasilimali hiyo hivyo wataongeza ushirikiano katika kuwalinda na kuwahifadhi.
Kwa upande wake Afisa Habari wa TAWA Beatus Maganja amesema Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imekuwa ikifanya mambo makubwa kwa wananchi kupitia taasisi hiyo, hivyo TAWA imejidhatiti kuuhabarisha umma wa watanzania kwa kufanya ziara wilaya kwa wilaya, vijiji kwa vijiji kuhakikisha wanaelewa umuhimu na faida za shughuli za uwindaji wa kitalii Nchini.
0 Maoni