TANAPA yajenga mabweni kukomesha ujauzito Sekondari Sitalike

 

Naibu Kamishna wa Uhifadhi na Maendeleo ya Biashara - TANAPA Herman Batiho amekagua bweni la wasichana jana Februari 23, 2024 katika Shule ya Sekondari Sitalike iliyoko Wilayani Mpanda katika mkoa wa Katavi linalojengwa na Shirika hilo ili kuwaondolea wanafunzi wa kike vishawishi vinavyosababisha mimba walivyokuwa wanakumbana navyo nyakati za kwenda shule na kurudi nyumbani.

Mradi huo wa bweni unaogharimu kiasi cha shilingi milioni 187.6 umekamilika kwa asilimia 99  huku ukiwa na vyumba 20 vyenye uwezo wa kulaza wanafunzi 80, matundu 5 ya vyoo na mabafu 5 yaliyomo ndani ya bweni hilo, huku asilimia 1 iliyobaki ni uingizwaji umeme unaotarajiwa kufanywa siku za usoni.

Kamishna Batiho alisema, "Wanafunzi wa kike wamekuwa ni wahanga wakubwa kutokana na vishawishi wanavyokutana navyo barabarani hivyo ujenzi wa bweni hili utaondoa adha hiyo na kuwafanya mabinti hawa wapate muda mwingi wa kujisomea na hatimaye kutimiza ndoto zao."

Naye, Mbunge wa Jimbo la Nsimbo Anna Lupembe alisema, "Ninaishukuru TANAPA kwa ujenzi wa bweni hili la kisasa na pia niliwaomba kutufanyia (wiring) katika nyuma za walimu wa shule ya Sekondari Sitalike, mkatekeleza."

Mkuu wa shule ya Sekondari Sitalike Mwl. Gervas M. Salehe alidokeza kuwa hapo awali wanafunzi wetu walikuwa wakikabiliwa na mimba zilizowapelekea kuacha shule kwa sababu ya kupanga maeneo yenye vishawishi  na maeneo hayo kukosa ulinzi kwa watoto wa kike na kuondoa ari ya kujisomea. Hali hii ilishusha kiwango cha elimu kwa kiasi kikubwa, ili kuwanusuru wanafunzi hao walimu waliitisha kikao cha wazazi na kukubaliana baadhi ya vyumba vya madarasa vitumike kama hostel na wazazi wachangie chakula, baada ya kufanya hivyo utoro ulipungua na ufaulu uliongezaka maradufu.

"Kulingana na madarasa hayo kutokukidhi vigezo vya kuwa mabweni kwa kukosa vitanda, ikabidi hostel hizo zifungwe, tokea hapo matokeo ya wanafunzi yameshuka sana, niwashukuru TANAPA kwa kuiona changamoto hii na kuifanyia kazi, nina imani mradi ukikamilika siku chache zijazo hata ufaulu  utakuwa ni mzuri sana," aliongeza Mwalimu huyo.

Baada ya ukaguzi wa mradi huo Kamishna Batiho pia, alifanya kikao na Menejimenti ya Hifadhi ya Taifa Katavi na kuwataka watumishi hao kuwa wabunifu katika utangazaji wa utalii na kuibua mazao mapya ya utalii ili kuvutia watalii wengi zaidi.

Hata hivyo, Kamanda wa Uhifadhi Kanda ya Kusini - TANAPA Steria Ndaga, alimshukuru kwa ujio wake na kumuahidi maagizo yote aliyoyatoa kuyafanyia kazi ili kuboresha utendaji kazi na kuongeza fursa za utangazaji kupitia vyombo mbalimbali vya habari na maonesho ya ndani na nje ya nchi ili kuvutia watalii wengi zaidi kuitembelea hifadhi hiyo inayosifika kuwa na viboko wengi.

Na. Jacob Kasiri- Mpanda

Chapisha Maoni

0 Maoni