Watumiaji wa barabara mkoani Dar es Salaam wameshauriwa
kutotumia barabara au vivuko ambavyo vimewekwa vizuizi katika kipindi hiki
ambacho mvua zinaendelea kunyesha nchini.
Wito huo umetolewa na Meneja wa TARURA Mkoa wa Dar es Salaam
Mhandisi Geofrey Mkinga wakati wa ukaguzi wa madaraja ya Luhufi na Tanganyika katika Wilaya ya
Kinondoni.
Mhandisi Mkinga amesema katika kipindi cha mvua barabara
nyingi huharibika zaidi na usalama kuwa mdogo hivyo wanaweka vibao watu
wasipite au wapite kwa tahadhari kwa maana barabara ni nyembamba
“Kwa kipindi hiki cha mvua, barabara nyingi zinakuwa
zimeharibika hivyo tunapoona usalama ni mdogo huwa tunaweka alama za tahadhali,
kwa hiyo tunaomba watumiaji wa barabara wazingatie hizo alama,” alisisitiza
Mhandisi Mkinga.
Ameongeza kusema kwamba kumekuwa na tabia kwa baadhi ya watu kutaka kupita kwa ngazi au magogo
vitendo ambavyo ni hatarishi.
"Tunafahamu hali ilivyo kwenye daraja hadi kufikia hayo maamuzi hivyo vile tulivyoweka
alama wasijaribu kupita kwani sio salama,”amesisitiza.
Akitolea mfano wa daraja la Msumi-Madale ambalo kwa sasa
hivi halipitiki kabisa na limefungwa ila bado kuna majaribio ya watu kutaka
kupita kwa magogo kitu ambacho ni
hatarishi.
Ameongeza kusema kwamba TARURA inaenda kujenga kivuko cha kutembea kwa miguu daraja la Msumi-Madale na litawasadia kuvuka ila wasijaribu kutumia njia zingine za kupanga mawe au miti kwani ni hatari kwa kuwa mvua zinaweza kunyesha na kusababisha kingo kuanguka na hivyo kuhatarisha maisha yao.
0 Maoni