TANAPA yanufaika na soko la kimkakati la utalii Zanzibar

 

Kamanda wa Uhifadhi Kanda ya Kusini - TANAPA, Steria Ndaga amesema uwepo wa Soko la Kimkakati la Utalii Zanzibar limechangia kwa kiasi kikubwa ongezeko la watalii katika Hifadhi za Taifa Tanzania (TANAPA) hususan, Hifadhi za Taifa Kanda ya Kusini na Mashariki ukilinganisha na miaka ya nyuma ambapo wageni wengi walikuwa wakitoka ukanda wa Kaskazini. Kamanda huyo ameyasema hayo leo tarehe 19.01.2024 kisiwani Zanzibar.

Akiwa katika Viwanja vya Maonesho ya 10 ya Biashara ya Kimataifa Fumba - Zanzibar, Kamanda Ndaga alisema,  "Maonesho haya ni sehemu ya mkakati wetu na wadau wa utalii kuhakikisha vifurushi vinavyouzwa katika Hifadhi za Taifa vinakuwa na idadi kubwa ya watalii wanaotumia muda mwingi hifadhini ili kuliongezea taifa mapato."

Itakumbukwa mwishoni mwa mwezi Agosti, 2023 Kamisheni ya Utalii Zanzibar (ZCT) na Bodi ya Utalii Tanzania (TTB) walisaini mkataba wa ushirikiano wa kutangaza vivutio vya utalii vilivyoko Tanzania bara na Visiwani ili kuongeza idadi kubwa zaidi ya watalii itakayofikia adhma ya watalii milioni 5 ifikapo Juni, 2026.

Naye, Kamanda wa Uhifadhi Kanda ya Mashariki - TANAPA, Massana Mwishawa alisema, "Lengo  la kufika Zanzibar kwenye maonesho haya ni kuwahamasisha wazawa na wageni kuchangamkia fursa za uwekezaji zinazopatikana ndani ya Hifadhi za Taifa Tanzania".

Aidha, Kamanda Mwishawa aliongeza kuwa uwekezaji unaotakiwa ndani ya hifadhi hizo ni pamoja na ujenzi wa malazi ya muda na ya kudumu ili kuongeza huduma za malazi kwa wageni ndani ya hifadhi. Hata hivyo aliendelea kufafanua kuwa kwa Kanda za Kusini na Mashariki kuna maeneo ya uwekezaji zaidi ya 60 huku Hifadhi ya Taifa Nyerere pekee ikiwa na idadi ya maeneo ya uwekezaji 38.

Kamishna Msaidizi wa Uhifadhi, Abel Mtui alisema, "Ongezeko la miundombinu ya barabara na viwanja vya ndege vimeimarishwa ili kuwezesha wageni kufika hifadhini bila adha yoyote. Kupitia  Mradi wa Serikali (REGROW) kuna takribani viwanja vinne vya ndege vyenye uwezo wa kutua ndege zenye uwezo wa kubeba abiria 50.

Vilevile, Kamishna Abel aliongeza kuwa kukamilika kwa viwanja vya ndege hivyo vitaongeza ufanisi na kuunganisha safari za wageni kutoka hifadhi moja kwenda nyingine. Hifadhi zitakazofaidika safari hizo ni Hifadhi za Taifa Mikumi, Ruaha, Nyerere, Saadan, Katavi, Udzungwa na Kitulo.

Sekta ya utalii kwa upande wa Tanzania bara inachangia kiasi cha asilimia 17 katika pato la Taifa, wakati kwa upande wa Zanzibar inachagia asilimia 30. Kwa mantiki hiyo uboreshaji wa miundombinu hiyo itaongeza idadi ya watalii nchini.

Na. Jacob Kasiri- Zanzibar

Chapisha Maoni

0 Maoni