Timu ya Maafisa Wandamizi
kutoka Vyombo vya Ulinzi na Usalama vya Zambia vinavyohusika na uzuiaji
ujangili wamefika nchini kwa lengo la kujifunza namna Tanzania ilivyofanikiwa
katika mapambano dhidi ujangili. Timu hiyo iko nchini kwa siku tano kuanzia Oktoba
29 hadi 4 Novemba, 2023.
Akizungumza mara baada ya
kutembelea Hifadhi ya Ziwa Manyara, Kamishna wa uzuiaji ujangili nchini Zambia,
Brigedia Jenerali, Herman Kamwita ambaye ni kiongozi wa ujumbe wa Zambia alisema
wamekuja kuona namnaTanzania ilivyofanikiwa kuendesha operesheni za kupambana
na ujangili na utekelezaji wa Mkakati wa Kupambana na Ujangili.
Alisema Kamisheni ya kudumu
ya Tanzania na Zambia ya Ulinzi na Usalama ilipendekeza Mamlaka ya nchi hizo
mbili kuwa na utaratibu wa kubadilisha uzoefu katika kulinda rasilimali za
wanyamapori na misitu.
Alisema wameweza kupitishwa
katika mbinu mbalimbali ambazo Tanzania inatumia katika kupambana na ujangili
na kuwa wamepanga kwenda kuzitumia wakirudi nchini kwao.
Aliongeza kuwa,
"tumepata fursa ya kwenda Hifadhi ya Ziwa Manyara na tumeona wanyama
mbalimbali na hii imedhihirisha namna wenzetu walivyopiga hatua kwenye uhifadhi
na niwahakikishie kuwa tutakwenda kutumia mbinu hizi ili kuimarisha sekta ya
utalii nchini kwetu.’’
Awali, Kaimu Mkurugenzi Msaidizi
wa Uzuiaji Ujangili na Mwenyekiti wa Kikosi Kazi Taifa Bw. Kiza Yusuph Baraga
alisema wamepokea ugeni kutoka Zambia na kuwa kupitia ziara hiyo, pande hizo
mbili zimebadilishana uzoefu.
" Madhuni na nia ya
nchi yetu ni kuendelea kutangaza utalii hasa kutokana na juhudi zilizofanywa na
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan za
kutangaza utalii kupitia Filamu ya The Royal Tour".
Ugeni huu pia, umepata fursa
ya kujionea vivutio vya utalii baada ya kutembelea Hifadhi ya Ziwa Manyara na
kushuhudia shughuli mbalimbali za utalii zinazoendelea ndani ya hifadhi hiyo.
Aidha, ugeni huo
umefurahishwa na mandhari nzuri na tunu tulizonazo na kuahidi kuwa sehemu ya
kutangaza utalii wetu nchini Zambia. Nitoe wito kwa watalii mbalimbali hususani
wa ndani na nje ya nchi kuja kutembelea vivutio vilivyopo Tanzania."
Kamanda wa Uhifadhi - Kanda
ya Kaskazini, Betrita Lyimo aliishukuru Wizara kwa ugeni huo kwa kutembelea
Hifadhi za Taifa Tarangire na Manyara kujionea hazina kubwa tuliojaliwa
Tanzania.
Aidha, Wakili Mwandamizi
Ofisi ya Mashtaka Makao Makuu ambaye pia ni Mratibu wa upelelezi, uendeshaji wa
kesi za makosa ya rushwa, udanganyifu na utakatishaji fedha sehemu ya makosa ya
mazingira na maliasili wa Kikosi cha Taifa cha Kupambana na Ujangili Theophil
Daniel Mutakyawa alisema, "kupokea ugeni huo na kubadilisha uzoefu ni
mwanzo wa ushirikiano katika kupambana na ujangili na pia kubadilishana taarifa
zinazohusiana na ulinzi wa Maliasili.
Mutakyawa aliongeza kuwa
makosa ya ujangili ni makosa yanayovuka mipaka, hivyo yanahitaji nguvu ya
pamoja ya kikanda katika kupambana na uhalifu huo mkubwa.
" Tumezungumza na
kuelewana kuwa sasa wanaporudi nchini kwao na sisi kubaki huku, utakuwa mwanzo
wa kuendelea kupeana uzoefu na taarifa ili tuweze kupambana na uhalifu
mkubwa."
Na John Bera
0 Maoni