Korea Kusini yanuwia kuleta vifaa tiba vya kisasa Muhimbili

 

Korea Kusini imeonesha nia yake ya kushirikiana na Hospitali ya Taifa Muhimbili katika kuboresha upatikanaji wa vifaa tiba vya uchunguzi vya kisasa kwa lengo la kuleta mabadiliko chanya ya utoaji huduma za afya.

Mwenyekiti wa Taasisi ya Global Cooperation Committee ya nchini Korea Kusini Bw. Jinil Kim amesema hayo wakati wa kikao na uongozi wa Muhimbili kilicholenga kushauriana namna ya kushirikiana ili kuleta maendeleo katika sekta ya afya hususani kwa upande wa vifaa tiba.

Bw. Kim ameeleza kwamba uwekezaji wa vifaa hivyo utaenda sambamba na kujengewa uwezo wataalamu namna bora ya kutumia vifaa na jinsi ya kuvifanyia ukarabati ili viweze kutumika kwa usahihi na kudumu kwa muda mrefu.

“Miaka 60 iliyopita Korea Kusini ilikua nyuma sana kimaendeleo, hivyo tunaamini endapo mkijidhatiti na tukashirikiana vema ninaiona Tanzania miaka 30 ijayo itakua imepiga hatua kubwa sana kimaendeleo,” amefafanua Bw. Kim.

Awali akizungumza katika kikao hicho, Kaimu Mkurugenzi Mtendaji Hospitali ya Taifa Muhimbili Dkt. Julieth Magandi amesema Tanzania imekua na ushirikiano mzuri na Korea Kusini tangu enzi za Hayati Baba wa Taifa Mwl. Julius Nyerere na hadi sasa uhusinao huo unaendelea kukua zaidi.

Ameongeza kuwa Korea Kusini imekua ikiisaidai Tanzania katika utekelezaji wa miradi mbalimbali ikiwemo ujenzi wa jengo la Hospitali ya Mloganzila, kusaidia vifaa tiba pamoja na kuendelea kuwajengea uwezo wataalamu wa ndani.

“Hatuna shaka na vifaa kutoka Korea Kusini kwakuwa vifaa vingi vinavyotumika MNH Mloganzila vimetoka Korea, bado wanatusaidia katika maeneo tofauti tofauti hivyo tunathamini mchango wao,” amesema Dkt. Magandi

Dkt. Magandi ameishukuru Korea Kusini kwa kuonyesha nia ya kuisaidia Muhimbili na kueleza kwamba MNH ipo tayari kushirikiana nao ili kuhakikisha lengo la kuboresha sekta ya afya linafikiwa kwa mafanikio makubwa.

Chapisha Maoni

0 Maoni