Umeme vijijini kuboresha viwango vya elimu- Kapinga

 

Naibu Waziri wa Nishati, Mhe. Judith Kapinga, amesema upatikanaji wa Umeme Vijijini kunaimarisha ubora wa elimu kwa shule za Msingi na Sekondari nchini.

Mhe. Kapinga amesema hayo wakati wa hafla ya kuwasha umeme kwa mara ya kwanza katika Kijiji cha Ukata wilayani Mbinga wakati wa ziara ya kukagua maendeleo ya Mradi wa Usambazaji wa umeme Vijijini Awamu ya Tatu Mzunguko wa pili Mkoani Ruvuma.

Amefafanua kwamba nia ya Serikali ni kuhakikisha mazingira ya ufundishaji na pamoja na ya kusomea kwa watoto wote nchini yanaimarishwa, pia wazazi wanasomesha watoto kwa jasho kwa mategemeo ya kupata viongozi bora wa kesho.

“Lengo la Serikali ni kuhakikisha tunaboresha mazingira ya ufundishaji ili walimu waweze kutumia vitendea kazi vinavyoendana na ulimwengu wa Sayansi na Teknolojia, haiwezekani mwalimu asiwe na Kompyuta wala na Printer akiwa anafundisha ili kusaidia mtoto tutakuwa tunalea taifa la aina gani? Kwahiyo ni lazima kuweka umeme sababu Dunia nzima inaenda na maendeleo ya sayansi na teknolojia,” alisisitiza Mhe. Kapinga.

Mhe. Kapinga aliwaeleza wananchi kuwa maendeleo ni hatua hivyo mradi wa REA unatekelezwa kwa awamu katika vijiji vyote nchini, na ifikapo Desemba 2023 vijiji vyote vitaunganishwa na umeme na kama kuna kitakachosalia kitaunganishwa wakati wa kuunganisha vijiji 22024.

Katika ziara hiyo Mhe. Kapinga aliambatana na Viongozi kutoka Wizara ya Nishati, Wakala wa Nishati Vijijini (REA) na Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO).

Chapisha Maoni

0 Maoni