Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF), unawahimiza wananchi
wa mkoa wa Mbeya na mikoa ya jirani kufika katika banda lake kwenye maonesho ya
Nane Nane yanayoendelea katika viwanja vya John Mwakangale ili kupata huduma za
upimaji na elimu ya afya bure.
Rai hiyo imetolewa na Meneja Uhusiano wa NHIF Bi. Anjela
Mziray ambaye ameeleza kuwa, suala la kujikinga na magonjwa yasiyoambukiza ni
la msingi kwa kila mtu na Mfuko unachangia juhudi za Serikali kwa kutoa huduma
za upimaji bure na kutoa elimu ya kuepukana na magonjwa hayo katika ushiriki
wake kwenye maonesho ya Nanenane.
"Tupo hapa kwenye viwanja vya John Mwakangale ndani ya
Mabanda ya Taasisi za Umma, tunawahimiza wananchi na washiriki wa maonesho haya
kufika hapa na kupima na kujua hali za Afya zao na kupata elimu mtindo bora wa
maisha ili kuepukana na magonjwa yasiyoambukiza," alisema Anjela.
Vipimo vinavyofanyika bandani hapo ni pamoja na Shinikizo la
damu, sukari na hali lishe na kisha wananchi kupatiwa matokeo ya vipimo.
0 Maoni